Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Iringa imezuia dhamana ya Mwenyekiti wa Mtandao Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo kwa sababu za usalama wake ikieleza kuwa bado maisha yake yapo hatarini.

Akizungumza leo Jumatano Machi 21, 2018 Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, John Mpitanjia amesema anaomba muda wa kusoma vifungu vya sheria mpaka Machi 26, 2018 ili kujihakikishia kama mtuhumiwa hatakuwa hatarini iwapo atapatiwa dhamana.

Akisoma mashkata yanayomkabili Nondo, Wakili wa Serikali, Abeid Mwandalamo amesema anatuhumiwa kwa makosa mawili.

Amesema kosa la kwanza ni  kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni Machi 7, 2018 akiwa eneo la Ubungo Dar es Salaam na kuzisambaza kupitia mtandao wa kijamii wa Whatsapp kwamba yupo hatarini.

Katika shtaka la pili, wakili huyo amesema Nondo ametoa  taarifa za uongo kwa mtumishi wa umma Mafinga alipokuwa anatoa taarifa kwa askari kwenye Kituo cha Polisi Mafinga kwa kusema kuwa alitekwa na watu wasiojulikana Dar es Salaam na kupelekwa kiwanda cha Pareto Mafinga. Hata hivyo, Nondo alikana mashtaka hayo.

Mwanadalamo amesema ushahidi bado haujakamilika hivyo wanaomba siku chache, kwa kipindi watakachokuwa wanafanya upelelezi mtuhumiwa asipewe dhamana.

Amedai kuwa kwa sababu bado wanafanya upelelezi kwa rafiki wake wa karibu, kama atapewa dhamana anaweza kuingilia na kuharibu upelelezi huo.

Wakili wa utetezi, Chance Luwoga amesema mashtaka aliyosomewa Nondo yanaruhusu kupewa dhamana.