JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya limemkamata Hamisi Ibrahim (15) akituhumiwa kumbaka na kumuua mtoto mwenye umri wa miaka sita.

 

Mtoto huyo alikuwa mwanafunzi wa darasa la kwanza na mwili wake ulitelekezwa kwenye pagale la nyumba jirani na nyumbani kwao, kwenye Kata ya Forest ya zamani jijini Mbeya.

 

Majirani wa marehemu wanasema mtoto huyo alikuwa akiishi na bibi yake na kabla ya mwili wake kupatikana juzi alitoweka nyumbani kwa siku mbili.

 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei, alisema jana kuwa polisi waliuondoa mwili wa marehemu juzi baada ya wasamaria wema kutoa taarifa.

 

Kamanda Matei alisema mtuhumiwa ni mkazi wa mtaa wa Kadege kata ya Forest jijini Mbeya.