Monday

tamthiliya inavyoisawiri jamii' Tamthiliya ya mbaya wetu ya ken walibora

0 comments

 

MBAYA WETU ( K. WALIBORA)NI TAMTHILIA INAYOSAWIRI MASUALA IBUKA. FAFANUA HUKU UKITOA MIFANO.

Maswala ibuka ni jumla ya mambo yanayoiathiri jamii moja kwa moja. Maswala kama haya yamesawiriwa vilivyo katika tamthilia ya Mbaya Wetu (2014).Masuala haya yanakusudia kutoa mafunzo maalumu kwa wasomaji hususan vijana.

Tunaongozwa na nadharia ya uhalisia. Lukacs (1963) anaeleza kuwa uhalisia sharti ujihusishe na mambo halisi yanayotokea katika mazingira halisi kupitia kwa wahusika. Wahusika ni vielelezo yakini vya binadamu wa kawaida kwa vile wao wanatumia lugha ya binadamu. Hali halisi ya wahusika na lugha wanayoitumia humwezesha mwanadamu kujifafanulia uwezo wake wa kutenda mambo na mtazamo wake kuhusu maisha.

Njogu (1997) anasema kuwa kazi ya msanii ni kiungo chake na jamii anayoilenga. Walibora anaibua masuala yanayoiathiri jamii ya kisasa katika ngazi zote za maisha. Masuala anayoyajadili yanalenga kumfanya binadamu awe mwanajamii mwema anayewajali wenzake. Anagusia nyanja za kijamii, kisiasa, kielimu, kitamaduni na kiuchumi. Nyanja hizi humsaidia binadamu kukuza hisia zake, tabia zake na kuyaelewa mazingira yake. Masuala ibuka yanayoibuliwa ni pamoja na Ufisadi, Ufeministi(Haki za wanawake) ukiukaji wa haki za binadamu(haki za wafungwa), matumizi ya dawa za kulevya na mapenzi na ndoa.

 

 

 

v  Ufisadi.

Ufisadi ni matumizi mabaya ya mali au raslimali za chama, shirika, watu au nchi kupitia rushwa kwa ajili ya kujinufaisha mwenyewe. Ufisadi umekuwa ni janga katika mataifa mengi. Obara (2015) anaeleza kuwa ufisadi unafaa kutangazwa kama janga la kitaifa nchini Kenya. Hii ni kutokana na kuongezeka kwa visa vya ufisadi. Kuna ufisadi bungeni ambapo wanakamati wa kamati ya uhasibu wanapokea hongo na kuandaa ripoti za kupotosha kisha majina ya watu wenye ushawishi wanaohusika na kashfa hii yanaondolewa. Ufisadi mwingine unashuhudiwa katika tume ya kupambana na ufisadi. Mwenyekiti anamsimamisha kazi naibu wa mkurugenzi kutokana na ukosefu wa maadili na anarudishwa na mkurugenzi siku hiyo hiyo. Pia, mradi wa vipakatalishi kwa watoto wa shule za msingi unasitishwa kwa kutofuatwa kwa kanuni za kisheria. Hali hii inasikitisha kwa vile inabainika kuwa taifa la Kenya linapoteza bilioni sitini na tisa kila mwaka kupitia kwa ufisadi.

 

Nalo shirika la AFP (2014) linaeleza kuwa  mahakama ya“Tel Aviv, Israel” inamhukumu waziri wa zamani miaka sita gerezani na kumtoza faini ya dola elfu mia mbili na tisini kwa kuhusika katika sakata ya ufisadi. Anachukua hongo ya dola elfu mia moja na sitini anapokuwa mamlakani ili kusitisha miradi ya umma.

Katika tamthilia , inatambulika  kuwa usifadi ni swala ambalo limekita mizizi katika ngazi mbalimbali za kijamii. Fiona ambaye ni mama mwuza buzaa na chang’aa katika eneo hili,amewalisha rushwa ili kuendeleza biashara yake haramu ya uuzaji Pombe haramu. Kwenye ukurasa wa 9 MTU II anasema:

[Kwa Fiona] Na hata kama humjui huyu polisi kwani hicho ni kitu  kwako wewe Fiona?... Ghalibu hukosi chochote cha kumlainisha moyo wake yabisi. Askari wote lao moja...... yaani bora mkono wende kinywani..... basi!

Hii ni ithibati kuwa Fiona amewarambishwa askari hawa mlungula hivyo basi upo uwezekano kuwa kuja kwao hakuna hofu yoyote ile kwa mwuzaji na wateja wake kwa kuwa dawa yao imo katika himaya ya Fiona.

 Swala hili la ufisadi vile vile lajitokeza wazi katika wahusika wengine kama njia ya kuuficha na kuuziba ukweli hasa katika misingi ya kifamilia. Jamii ya Mzee Temba inajikita katika njia-panda wakati mwanao kitindamimba Matari anapotiwa mbaronikwa kumwibia nduguye, Tonge ng’ombe wa maziwa na kumwuzia Jefule mwenye bucha. Temba anaingiwa na wasiwasi kwa kukosa la kufanya. Anaamua kwenda kwa Tonge ili amrai kukubali kuiondoa kesi kutoka mikononi mwa polisi hadi nyumbani ili waelewana kama jamii.Kwenye ukurasa wa 32 Mzee Temba anasema:-

............ Ni kweli Matari kakowa manza, lakini yeye Tonge asikubali polisi wampeleke nduduye mahakamani. Hiyo haihalisi......Hata kidogo haihalisi.....Nitamnasihi Tonge anasihike, tuje pamoja naye kwenye kituo cha polisi tuwambie polisi mambo haya tuyamalizie nyumbani....

Kwa yakini mzee Temba alifanya vivyo hivyo ingawa tarajio lake halikuwa swari tu kama alivyotaka yeye. Tonge kwa upande wake alihitaji sheria ifuatwe ili Matari na Jefule wawe mfano mwema kwa wale walio na tabia kama zao.Waaidha familia ya Jefule kupitia kwa Bi. Mkubwa. Kwenye ukurasa wa 62 bibi huyu asema:-

 

[Baada ya kusalimiana mikononi]Mzee Temba, nimekujia kadha si kadha wa kadha. Hebu sikiliza.Watu wa Jefule wamenituma nije niseme nanyi.Wako radhi kulipa fidia kesi imalizikie papa hapa kijijini isiende mahakamani mjini.

Kupitia kwake inadhihirika wazi kuwa jamii ya Jefule iko tayari kumhonga Tonge ng’ombe mmoja ili kesi hiyo imalizikie nyumbani. Hata hivyo masharti ya Tonge yalikuwa marudishe ng’ombe wote sita waliopata kuibwa.

Tonge akiwa katika kituo cha polisi ili kuona kuwa walitiwa mbaroni wanakumbana vilivyo na mkono wa sheria, anakutana ana kwa ana na kizingiti kingine kutoka kwenye maafisa wa polisi.

Kwa kweli adara ya polisi imekuwa katika mstari wa mbele katika swala zima la ufisadi kwa kuliabudu. Hapa nchini Kenya idara hii imeibuka kidedea katika ufisadi.

Kupitia kwa Johnstone Kavuludi,Mwenyekiti wa Tume ya Huduma za polisi(PSC) na kama ilivyoripotiwa na idhaa ya BBC Oktoba 2015 Takriban maafisa 63 wa kikosi cha polisi nchini Kenya walifutwa kazi kufuatia madai ya kuhusika na ufisadi.

Msemaji wa polisi alikuwa  miongoni mwa wale waliofutwa kazi kulingana na mwandishi wa BBC Joseph Odhiambo.

Tume ya huduma za maafisa wa polisi iliwafuta kazi maafisa hao baada ya kuwakagua maafisa 1,300 kwa kipindi cha miezi 14.

Mbali na msemaji wa kikosi cha polisi wa utawala Masoud Mwinyi,wengi wa wale waliosimamishwa kazi walitoka katika idara ya trafiki.

Mwenyekiti wa tume hiyo Johnston Kavuludi alisema kuwa wakati wa ukaguzi huo waligundua kwamba maafisa wa vyeo vya chini wanaofanya kazi katika idara hiyo walikuwa wakituma kiwango cha fedha wanachopata kwa maafisa wanaowasimamia kupitia simu zao.

Lakini wakenya pia wamelaumiwa kwa kuchanga kuongezeka ufisadi kwenye idara hiyo aidha kwa kutojua au kwa kupuuza sheria. Naibu mkurugenzi wa tume ya maadili na kupambana na ufisadi Michael Mubea anasema wananchi wanapaswa kutokubali kutoa hongo na badala yake kutoa bondi inavyohitajika kisheria kunapotokea makosa.

Kule Tanzania mambo ni yale yale. Kupitia vile vile kwenye habari za BBC Januari 2,2015 ilitangazwa wazi kuwa idara ya polisi ilikuwa ikiongoza katika visa vya ufisadi.Ripoti hiyo ilisema kuwa  idara ya polisi ndiyo taasisi inayochukua hongo zaidi nchini Tanzania kulingana na ripoti ya ufisadi katika jumuiya ya Afrika mashariki.

Ripoti hiyo ilisema kuwa maafisa wa polisi walipokea asilimia 25 ya hongo zote zilizotolewa kwa wafanyikazi wa taasisi za uma mwaka uliopita.

Ya pili ni idara ya mahakama,ambayo wafanyikazi wake walitia mfukoni asilimia 18 ya hongo,huku mashirika yalio na majukumu ya usajili na utoaji wa leseni yakiwa katika nafasi ya tatu kwa asilimia 10.

kwa mujibu wa gazeti la The Citizen, Idara ya Polisi nchini Tanzania ilitajwa kuwa ya tatu kwa ufisadi katika jumuiya ya Afrika Mashariki.

Polisi wa Uganda wanaongoza wakifuatiwa na wale wa Kenya katika nafasi ya pili na wale wa Burundi wakiwa katika nafasi ya nne.

Kulingana na ripoti hiyo maafisa wa polisi wa Rwanda ndio wasiochukua hongo ya juu Afrika Mashariki.

Utafiti huo ulifanywa mwezi Julai na Agosti mwaka  wa 2014 na shirika la lenye na maslahi ya kimaendeleo barani afrika ForDIA likishirikiana na Jukwaa la uwazi nchini tanzania Trafo.

 

Kwenye tamthilia ya Mbaya Wetu, polisi vile vile wamejitokeza wazi kuwa wanyonyaji wa wananchi. Hii inadhihirika wazi wakati Tonge anapoambiwa kuwa na ASKARI 1 kuwa:-

Nilikwambia karandinga letu halina hata tone la mafuta.Sisini maaskari waaminifu, hatupendi kuwarubuni watu.Mafuta yaliyomo ni ya kuwapeleka wanywaji wa Pombe haramu mjini kushatakiwa mahakamani, Kwa hivi sasa hatuna washukiwa wa ulevi.....Wataka nikuambie mara ngapi nawe? Labda nyie mtumie gari lenu.

Huu umekuwa msemo wa kawaida wakati raia wanapohitaji huduma kutoka kwa polisi.Polisi hupenda sana kusingizia kukosekana kwa mafuta ya gari. Ajabu ni kwamba ukiwaarifu kuwa wakubali upeleke gari lao kwa mafuta halisi, hamtaelewana kabisa. Sarakasi ni kuwa ukijitolea kuwapa hela za mafuta ya gari, karandinga huenda ulikotaka bila kupitia kwenye kituo cha mafuta!Iwapo utakuwa mgumu basi utapewa vitisho vya kila namna.

 

Kwenye kituo cha polisi pamewekwa kibao kipana kilichoandikwa ilani “HAPA SI MAHALI PA KITU KIDOGO”.Ilani hii ni kinyume cha mambo. Hiiinadhihirika wazi wakati Tonge anaposhinikizwa kulipia huduma kwa kuelekezwa kufafanua maana ya ilani hiyo na Askari II. Anapotoa noti kadhaa na kumpa Askari II kisha kuuliza iwapo ametimiza masharti,madahalo unadhihirisha wazi kuwa ilani hiyo si haramu bali halali kwani wanaiboronga maana yake ili kuitumia kuwaibia raia.

Tonge: Sawa?

 Askari II:Si sawa.

Tonge: Kwa nini?

Askari II:Wajua kusoma

Tonge: Kwa nini?....Mimi mtu aliyesoma sijui kusoma?

Askari II:Basi soma pale.[Anamwonyesha ilani “HAPA SI MAHALI PA KITU            KIDOGO”

Tonge:     Hapa si pahali pa kitu kidogo!

Askari II:  Inakuelea?

Tonge:      Yaani hongo hairuhusiwi hapa.

 

Askari II:    Hata kidogo.Kumbe elimu mnayosoma haiwasaidii kitu. Ilani kidogo tu, inakushindwa kuelewa. Maanake hasa ni kwamba hatukubali sisi kitu kidogo; twakubali kitu kikubwa tu.......

Akiwa kwenye kituo cha polisi kumletea Matari chakula(mkate na soda) Fiona anakosa kuelewana na Askari II ambaye nia yake kwa Fiona ilikuwa potofu huku akikejeli Fiona kutokana na tuhuma zake mwenyewe kuwa Fiona na Matari ni wapenzi. Fiona kwa upande wake anayapinga hayo na kupitia kwake tunajifunza kuwa amekuwa katika mstari wa mbele kuwahonga Askari polisi. Hii inadhihirika wazi anaposema kwenye ukurasa wa 53:

Lo! Mara ngapi nikulipeni hongo?......Mara ngapi?....Eeh?....Mbona hata mwaweza kujenga makasri kwa mapesa ninayowahonga kila uchao.

Askari I naye anakiri kwa kusema:

                                    “Ahaa! Hilosikatai.Nimekula pesa zako kilamwezi kidogo kidogo”.

Ni wazi kuwa idara hii ya polisi imeamua kukejeli ilani za utendajikazi kwa kulazimisha umma kuzielewa kinyume.

 

v  UKIUKAJI WA HAKI ZA BINADAMU(HAKI ZA WAFUNGWA.)

Haki ni kiungo muhimu katika utawala wa kidemokrasia na ndiyo msingi wa sera za kijamii, kiuchumi na kitamaduni. Serikali ina wajibu wa kutambua, kuheshimu na kulinda haki hizi. Haki za binadamu sharti zitiliwe maanani ili kuiendeleza jamii. Njogu (2007) anafafanua haki za makundi mbalimbali kama vile wafanyakazi, wafungwa, walemavu na watoto.

 

Wafungwa wana haki ya kupewa mahitaji msingi kama binadamu wengine. Haki hizo ni: kuishi, kupata mahitaji msingi kama chakula, makazi na mavazi, kuheshimiwa na kupewa uhuru wa kujieleza, kumiliki mali na kutangamana na wenzake. Visa vya ukiukaji wa haki za wafungwa vinashuhudiwa katika jamii yetu. Makala ya “Magereza yetu yasifurike,” 2014, ukurasa wa 11, yanaeleza kuwa idadi ya wafungwa katika magereza nchini Kenya inafaa kupunguzwa. Wafungwa hawapati chakula cha kutosha, mazingira ni duni na huduma za afya ni duni. Nalo shirika la AFP (2014) lilieleza kuwa mfungwa mmoja Marekani alizuiliwa kuhudhuria mazishi ya mama yake.

 

Kwenye tamthilia wafungwa au watuhumiwa hawapewi haki yao. Mahali wanakowekwa hapafai hata kidogo.Hii inadhihirika wazi kupitia kwa Matari ukurasa wa 50:

Matari:[ Kwa askari]........Nimeathirika sana nina njaa kibao, sijala kitu tangu usiku wa kuamkia jana, sikwambii huku kuliwa na chawa na viroboto kwenye seli hii.

Wakati Matari anapoomba idhini ya kuenda msalani, jibu analopata ni ishara tosha kuwa afya ya wafungwa na washtumiwa imo hatarini kabisa. Hii inadhihirika kupitia kwa mdahalo huu ukurasa wa 51:

Matari:Afande nataka mwenda kujisaidia.

Askari I: Tumia ndoo iliyomo humo ndani.

Matari: Ndoo imejaa.

Askari I: Nani alikuambieni muijaze ndoo haraka?Wacha kunitumia kama kopola msalani.Nitakutandika ugeuke rangi uwe mweusi kama kunguru.

Hii ni pamoja na kutowapa chakula kwenye seli na iwapo wataletewa basi Askari wanakila wao wenyewe. Fiona anapomletea Matari soda na mkate, Askari I anaanza kuula mwenyewe pasipokujua kuwa mfungwa anafaa apewe haki yake. Kwake Askari huyu ni kuwa mfungwa au mtuhumiwa hana haki yoyote ya kula akiwa kituoni.(uk. 53-54).

 

v  HAKI ZA WANAWAKE

Wanawake na wanaume wana haki sawa. Hata hivyo kutokana na sababu mbalimbali wanawake hawakuweza kufaidi haki zao kama wanaume. Mikataba mbalimbali imepitishwa kuhakikisha wanawake wanafaidi haki sawa na wanaume. Pia kuna sheria mbalimbali za nchi zinazolinda haki za wanawake.

 

Ikumbukwe kuwa mikataba mikuu ya haki za binadamu imeweka kanuni kuu ya kutobaguliwa katika kufaidi haki za binadamu kwa misingi ya jinsi, dini, kabila, rangi, umri, utaifa, na kadhalika. Hii inamaanisha kuwa haki za binadamu zapaswa watu wote wazifaidi bila ubaguzi wa aina yoyote.

Hata hivyo bado baadhi ya makundi ya watu katika jamii hasa wanawake, hawakuweza kupewa nafasi sawa kufaidi haki zao. Ndio maana juhudi zimefanyika na zinaendelea kufanyika katika ngazi ya kimataifa, barani Afrika na hata hapa nchini Tanzania kuhakikisha kwamba haki za wanawake zinalindwa.

 

Mikataba ya Kimataifa inayolinda Haki za Wanawake

Mkataba wa Kimataifa wa Kuondoa Aina Zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake wa Mwaka 1979.

Mkataba wa kimataifa wa kuondoa aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake au kwa jina jingine unajulikana kama ‘Mkataba wa Wanawake’ ndio mkataba mkuu unaolinda haki za wanawake duniani. Mkataba huu ulikubaliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, mwaka 1979 na ulianza kazi tarehe 3 Septemba, 1981. Tanzania imesaini na kuukubali mkataba huu tarehe 19/09/1985.

Mkataba huu umelenga kuhakikisha kuwa wanaume na wanawake wanafaidika kwa usawa na fursa za kiuchumi, kijamii, kitamaduni, kiraia na kisiasa kwa kuondoa aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake.

Mkataba nyongeza wa Haki za Wanawake Barani Afrika wa mwaka 2003.

Mkataba huu umepitishwa na wakuu wa nchi na serikali za Afrika mwaka 2003 huko Maputo, Msumbiji. Hadi Agosti 2004, ni nchi nne (4) tu za Umoja Afrika zilizoridhia mkataba huu.

Kwa ujumla, mkataba huu ambao pia unajulikana kama “Mkataba wa Maputo” unalinda haki za wanawake wa barani Afrika.

 

Na mojawapo ya sifa yake kuu ni kutamka wazi kwa mara ya kwanza katika sheria za kimataifa haki za uzazi za wanawake ikiwemo kutoa mimba kama imepatikana kutokana na kubakwa au inamuweka hatarini mwanamke. Pia mkataba huu nyongeza unapiga marufuku ukeketaji wa wanawake. Kwa ujumla, mkataba wa nyongeza wa haki za wanawake wa Afrika unaweka majukumu kwa nchi na serikali za Afrika kulinda na kutekeleza haki za wanawake katika nchi zao. Ubaguzi wowote wa kijinsia ni kinyume cha Katiba ya nchi.

 

Ubaguzi unaokatazwa na Katiba unaweza kuwa dhidi ya rangi, kabila, jinsi, utaifa, mahali mtu alipozaliwa au hali ya maisha ya mtu. Kwa maana nyingine, katiba ya nchi inatoa haki sawa kwa wanaume na wanawake nchini Kenya katika Nyanja zote za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.

Baadhi ya mikakati wanajamii wanaweza kuitumia kuhamasisha ulinzi wa haki za wanawake katika jamii ni kama ifuatayo:-

Ø  Kutoa elimu kwa jamii (wanaume, wanawake, viongozi wa kimila, viongozi wa dini, walemavu n.k) kuachana kabisa na mila na desturi zinazomkandamiza, kumuumiza na kumbagua mwanamke.

Ø   Kutoa elimu katika ngazi ya familia na kaya juu ya haki za wanawake

Ø   Elimu hii itolewe kwenye mikutano ya vijiji, mashuleni, masokoni, gulioni, nyumbani, kwenye vikundi vya kuweka na kukopa, vyama vya ushirika n.k

Ø   Kutoa taarifa kwa vyombo husika pale haki za wanawake zinapovunjwa. Vyombo hivi ni pamoja na serikali ya mtaa, polisi, idara ya ustawi wa jamii, asasi za kiraia zinazopinga ukatili dhidi ya wanawake n.k.

Ø   Kushirikisha wanaume kwenye ulinzi wa haki za wanawake

Kumbuka wanawake wanayo haki ya kufaidi matunda ya utu/ ubinadamu wao sawa kabisa na wanaume. Baadhi ya mifano ya haki za wanawake ni:

Ø  haki ya kuishi, uhuru na usalama wa maisha yake 

Ø  haki ya kutobaguliwa katika jamii kwa sababu tu ya jinsi yake

Ø   haki ya kutotendewa kinyama au kikatili 

Ø  haki ya kumiliki ardhi na/au mali nyingine yeyote inayohamishika na isiyohamishika

Ø   haki ya uhuru wa kutoa na kueleza maoni yake

Ø  haki ya kushiriki katika kutoa maamuzi yahusuyo maisha yake, familia yake na jamii yake

Ø   haki ya kupata elimu.

Ø  haki ya kupata fursa sawa ya ajira na kulipwa ujira unaostahiki

Ø   Haki ya afya na afya ya uzazi

Ø  haki ya kupumzika kwa likizo ya uzazi.

Katika tahthilia, mwanamke amenyang’anywa haki yake katika hali mbalimbali. Mifano ya wanawake walioathirika katika ukosaji wa  haki yao katika jamii husika ni pamoja na Fiona, Lila,Mamaye Matari.

Jamii hii inamwona mwanamke kama chombo cha kumfurahisha tu mwanamume na hakuna cha mno.Matari anaamua kumchukua Fiona kama chombo chake cha kumrithisha kimapenzi. Hali hii inadhihirika wazi wakati Fiona anapenda kwenye kituo cha polisi akiwa na nia ya kumpelekea Matari chakula Askari I anasema:

Nimesema hapewi mkate na soda. Seli sio mahali pa watu walio ndani na walio nje kuonyeshana mapenzi.(uk.52)

Anazidi kunadi kuwa:

Na mpenzi wako nani? Tangu hapo nakuona mwanamke mzima nikitakacho hunipi. Kumbe umezuzuzuliwa na hilijambazi hatari mburumatari liitwalo Matari.Hili jambazi ndilo dawa ya moyo wako sio?(uk 53)

Kupitia kwa usemi wa Askari I ni ishara tosha kuwa hata yeye humwona mwanamke tu kama chombo tu cha kutimiza haja za wanaume hakuna jingine.

Askari I anazidi kwa kusema kuwa:-

........................... Nitapeleka salamu kwa dadako bila shaka kama yeye ni mzuri wa kugawa tenda na kufungasha vilivyo kama mwanamke halisi wa Kiafrika. Sivipendi visichana vya kisasa vinavyowaiga Wazungu na kujikondesha vikabaki kama shingo za flamingo.Namtaka mwanamke aliyeunga Sawasawa.....aliyekula akashiba......Nikipata nafasi nitamtafuta huyu dadako. Akinisikiza utapata mkate na soda.

Hata Matari kwa upande wake anamwona Vero, shemegiye kama chombo cha kujifurahisha. Hali hii ndiyo iliyopelekea Vero kupata uja uzito kutoka kwa Matari ambaye ni shemeji yake. Katika ukurasa wa 56 Matari anakiri haya kwa kusema:

Afande umeskia?Ee?Shemeji asimwambie mtu kwamba mimindiye niliyemtunga mimba.

Tabia zake Matari zinamwelekeza kumbaka Fiona pindi alipotoka seli baada ya kuachiliwa akaenda moja kwa moja kwa Fiona ambapo alimtaka amrudishie zile pesa alizomwibia Lila kabla ya kushikwa. Fiona alimwarifu kuwa hazikuwa jambo ambalo Matari hakulikubali.

Matari akiwa na Fiona chemba kunasikika sauti ya Fiona ikilia:

Uwiiiiii! Uwiiiiii!Wacha kunibaka. Wacha kunibaka. Wacha kuniibia. Nduli wewe....Kama wataka kuniua niue.

Kitendo hiki ndicho kilichomrudisha Matari kwenye mikono ya sheria baada ya umati kutaka kumpiga kitutu. Inasemekana kuwa Fiona ndiye aliyetoa mafuta ya gari la polisi.

 

Mwananamke pia amechorwa kama kiumbe ambacho hakiwezi kukubalika kutoa ushairi na kufanya maamuzi katika jamii.Kupitia kwa MAMA inaonyesha kuwa Temba hampi sikio hata kidogo katika mijadala yake. Hii inadhihirika kupitia usemezano huu(uk 60):

Temba:[Anapuuza mikemeo ya Mama. Anaketi Mkabala na mtoto wa meza]. Lila

Lila: Naam baba.

Temba:Nenda ukamwambie Mjakazi aniletee chakula.Nina njaa.[Lila anaondoka]

Mama: Nauliza mwanangu yu wapi?

Temba:[Anaita] Lila!

Lila: [Kutoka nje ya jukwaa] Labeka!Baba.

Temba: Mwambie Mjakazi asitie chumvi nyingi kwenye chakula. Kazoea vibaya sana huyu.

Lila: Ndiyo baba.

Temba: [Kwa Lila] Na chsakula apashe moto vya kutosha

Mazungumzo haya yanamweka Mama katika wingi wa wasiwasi ikibainika wazi kuwa mwanawe kitindamimba yumo hatarini. Hata hivyo kupitia kwa Temba tunabaini wazi kuwa jamii haiku tayari kumkubali mwanamke kikamilifu katika utoaji wa mielekeo.

 

Kwa kifupi tunaweza kusema kuwa haki za wanawake ni haki za binadamu. Kwani mwanamke anastahili kulindwa na kuheshimiwa utu wake na kufaidi fursa zote zilizoko katika jamii yake kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii.

 

v  MAPENZI NA NDOA

Burke (1999) anaeleza kuwa baadhi ya watu hujiingiza katika uhusiano kutokana na msukumo wa ubinafsi na unafiki. Kuna ukosefu wa mapenzi ya dhati miongoni mwa wanajamii. Katika tamthilia , tunaelezwa kuwa mapenzi baina ya Matari  na Fiona  ni karubandika tu .Hii ni kwa sababu  Fiona anafaidika tu kwa kuwa baada ya Matari kuwaibia watu basi yeye yu tayari kuzipokea zile pesa ambpo Matari na walevi wenziwe huzipunguza kidogo kidogo tu. Hii inadhihirika wazi kwa kubainika wazi kuwa babada ya Matari kumwibia dada yake Lila bunda lake la noti anazibeba hela zote hizo kwa Fiona ambaye alizimenya zote baabda ya Matari kutowa mbaroni mwanzo. Ugomvi wao kuhusu akiba ya pesa hizo ndio uliokuwa sababu ya Matari kurudi mikononi mwa polisi.

 

Vilevile mapenzi yaliyojitokeza kati ya Matari na Vero yanaelekea kuisambaratisha jamii ya Temba hasa ile ya mwanawe , Tonge. Hii ni kwa sababu licha ya Matari na Vero kuwa mashemeji wameenda hatua ya kuwa wapenzi kisha mimba ikapatikana.

 

Mapenzi na ndoa huambatana sako kwa bako. Ndoa ni kiungo muhimu katika jamii. Hii ni kwa sababu huchukuliwa kama kilele cha ukuaji wa mtu. Al- Farsy (1969) anafafanua kuwa ndoa inastahili kupewa umuhimu na udhati na wahusika kwani huwaweka pamoja milele; mume na mke ni washirika wa milele na sharti wawe tayari kwa majukumu yanayoandamana na ndoa. Ongachi (2014) anaeleza kuwa ni vyema kuweka wazi matarajio kabla ya kufunga ndoa ili kupunguza misukosuko. Katika jamii, tuanashuhudia visa vya ukatili katika ndoa vinavyotokana na ukosefu wa mapenzi ya dhati. Matheka (2014) anasimulia kisa cha mwanamke mmoja anayemdunga mume wake kisu baada ya ugomvi baina yao. Ugomvi huo unatokana na mwanamume huyo kukosa kuwajibika katika kuilisha familia yake. Mke wake analamika kuwa anamwachia majukumu ya kuwalea watoto wao. Mwanamume huyo anapata majeraha mabaya. Naye Muiruri (2015) anaeleza kisa cha mwanamume anayechomwa na mke wake kwa sababu ya kukosa kuleta unga mjini Kirinyaga, Kenya. Mwanamume huyo anazama katika ulevi na kuisahau familia yake. Mke wake anasema kuwa anaamua kumchoma ili kumshurutishe ayatekeleze majukumu yake kama mume na baba ya watoto wake. Katika tamthilia tunabainisha kuwa ndoa kati ya Tonge na Vero inakosa Uaminifu. Tonge yuko mjini kusaka tonge huku mkewe, Vero kuwa na jicho la nje hadi kupachikwa mimba na Matari ambaye ni shemeji yake.

 

Waaidha ushirikino ni swala muhimu sana katika ndoa. Hata hivyo jamii nyingi hukosa kufahamu hili. Katika tamthilia inaonekana wazi kuwa Temba hana nafasi ya kumpa mkewe sikio ili atoe mapendekezo katika jamii. Ameona kuwa mawaidha ya Mama hayana msingi wowote pasipokujua kuwa pasi mchango wa kila mmoja jamii haina nguvu.

 

v  HAKI YA  MALEZI KWA WATOTO

Watoto wana hadhi maalumu katika jamii na ni jukumu la familia na serikali kuwaelimisha na kuwalinda. Haki za watoto kama vile malezi bora, kulindwa dhidi ya dhiki, kupewa elimu, kutofanyishwa kazi nzito na kupewa matibabu.

Mama na baba mtoto wana haki sawa katika kulinda na kuyakidhi mahitaji ya mtoto. Kila mtoto ana haki ya kulelewa na wazazi halisi au wazazi mbadala iwapo wazazi wake halisi hawajimudu kihali, kiafya au wameaga. Hakuna mzazi anayefaa kujitenga kwa vile mtoto ni wa wote.

Katika tamthilia inathibitika wazi kuwa mzigo mkubwa wa kumlea Matari uliachiwa Mama huku Temba akijitenga kabisa. Hii inajitokeza kupitia semi mbalimbali wakati Matari anapotiwa mbaroni kwa kosa la kumwibia Tonge ng’ombe wake. Tonge kwenye ukurasa wa 62 anasema:

Mama hii leo mwanilaumu lakini ukweli ni kwamba matendo ya Matari ni tokeo la kutendekezwa. Ni kosa lenu.Si langu.

Kupitia dondoo hili ni wazi kuwa Matari hakuweza kuipata haki yake ya kupewa malezi ifaavyo ndipo awe mkamilifu kimaandili. Kudekezwa huku kunapita mipaka kiasi kuwa hata anapokosea hadharani, Mama yupo katika mstari wa mbele kulikana hilo waziwazi.

Temba kwenye ukurasa wa 66 anathibitisha kuwa kukosekana kwa juhudi za wote wawili katika malezi ya mtoto ndiko kunakoleta balaa. Anaamini kuwa Matari amedekezwa pakubwa na Mama ndio maana hakui na kuwa mwanajamii bora. Anasema hivi:-

Basi endelea kumdekeza adekezwe. Yatakuja kukutokea puani.Wacha nende      zangu.........

Hii ni wazi kuwa swala la malezi ya Matari liliingia mchanga kwa kukosa maafikiano kati ya Wazazi kuhusu namna ya kuwalea wanao. Huenda ikawa ndio sababu Ndugu zake wakubwa(Tonge na Lila) waliweza kusoma kuliko Matari.

 

Suala la watoto kuzaliwa nje ya ndoa linashuhudiwa katika jamii ya kisasa. Sheria inaeleza kuwa watoto wanaozaliwa katika ndoa au nje ya ndoa wana haki sawa. Kila jamii ina mitazamo tofauti kuhusu watoto wanaozaliwa nje ya ndoa. Kakah (2014) anasimulia kisa cha kiongozi mmoja nchini Kenya, anayemtelekeza mtoto anayemzaa nje ya ndoa. Hili ni dhihirisho kuwa kumzaa mtoto nje ya ndoa katika jamii kunachukuliwa kuwa ni haramu. Baadhi ya wanaume hawataki kuhusihwa na watoto hao kwa sababu wanawaona kama si halali. Jukumu la kumlea linawachiwa mwanamke.

 

Kwenye tamthilia upo uwezekano mkubwa kuwa ulezi wa mtoto atakayezaliwa na Vero utaleta kizungumkuti. Hii ni mimba iliyotungwa na Matari ikizingatiwa kuwa Tonge, nduguye hana habari. Tunakisia kuwa iwapo habari hizi zitamkaa akilini Tonge ambapo upo uwezekano mkubwa kwa kuwa wanakijiji wameanza kuyasoma chini ya maji, basi hatari ipo njiani. Uwezekano mkubwa upo wa Vero kutafuta namna ya kumlea huyo mtoto pindi tu atakapozaliwa.

v  MATUMIZI YA DAWA ZA KULEVYA.

Katika tamthilia hii Pombe imetawala pakubwa. Mwanzoni tu mwa tamthilia inapoanza inadhihirika wazi kuwa Pombe imewaathiri watu wengi mno.Tunakumbana moja kwa moja na Fiona ambaye ni mama mwuzaji wa Pombe haramu, buzaa na chang’aa.

Makao yake hushona walevi kucha kutwa wakiwa na ari ya kuburudika kwa kileo chao wakipendacho.

Hata hivyo Pombe hii imekuwa na madhara mbalimbali kwao kwenye ndoa zao. Kwenye ukurasa wa 2 Mtu I anasema haya:-

Hapana........Uache kumsifu Fiona bure bwana.Mgema akisifiwa tembo hulitia maji.Ama hujasikia wewe watu siku hizi wanapofuka wanywapo Pombe?

 

Dondoo hili litakupa mwanya na mwangaza wa kufahamu kuwa Pombe haramu ina uharamu wake kwenye afya za watumizi hasa viungo vyao ambapo wengine hujikuta kuwa macho yao hayafanyi kazi kabisa. Hali kama hii ilishuhudiwa na inazidi kushuhudiwa nchini Kenya ambapo walevi huathiriwa pakubwa na Pombe haramu wanayoitumia.

 

Waaidha walevi wengi hasa wanaume hutelekeza majukumu yao ya kindoa kwa wake zao.Hali kama hii hufanya familia nyingi kuvunjika kwa kuwa mke huonakuwa haipo haja kuishi na mume ambaye tayari ameyarudisha majembe ghalani mapema. Wengi wa wanawake huingilia ukahaba au mipango ya kando kama inavyoshamiri kucha kutwa katika jamii zetu.

Wanawake wengi katika kaunti zinazoathirika kwa Pombe wameonekana wakiandamana kuililia serikali iingilie kati na kuona kuwa Pombe haramu imepigwa marufuku katika eneo lao na iwapo hilo halitafanyika basi wanatishia kuhamia kwingineko waliko wanaume kamili!

 

Walevi wengi wanapokosa pesa za kununua Pombe, wengi wao hujikuta wakiiba ili waweze kugharamia kileo. Katika tamthilia tunaona kuwa Matari anaashinikizwa na raghba yake ya Pombe na kuwa mwizi sugu na asiye na haya wala soni. Anamwibia dada yake, Lila waziwazi pesa zake na kumpelekea kahaba wake muuzaji Pombe ambapo anaonekana akiwaburudisha walevi wenzake.

Matari anakiri wazi kuwa ndiye aliyeziiba pesa za dadaye kwa kuwema haya kwenye ukurasa wa 18:-

Fedha zako nitakulipa.Saa hii sina, Nipemuda tu.Lakini la kumwambia Mama usimwambie.....

Kwa hivyo ulevi na wizi ni pacha kiasi kwamba hutegemeana ilimtumizi aweze kutimiza ari yake ya kulewa. Hayo hayakukomea hapo.Matari vile vile ndiye aliyekuwa akiving’oavipuri kutoka kwenye trekta  lao usiku na kuviuza ili aweze kupata pesa za ulevini.

Katika ukurasa wa 19 Mama anasema haya kwa Matari:-

Wajua. Usiniambie hujui kwamba yupomtu wa mkono aliyeviiba vitu kwenye trekta na kuuza kimojabaada ya kingine.......Trekta inaegeshwa usiku ikiwa na kila kitu. Hapa kwtu usiku mbwa wakali sana hathubutu mtu ajinabi kuingia. Asubui ikifika vitu kadhaa havipo...Sharti awe mmoja wetu..Mwizi wa vipuri labda ni babako mwenyewe,mimiau wewe mwanangu.Mmoja wetu ana mkono.

Anapoachiliwa huru kutoka kwenye kituo cha polisi, Matari anazidi kuonyesha kuwa ameathiriwa na wizi kisingizio kikiwa uchu wa Pombe.Anaamua kukwapua nguo za Askari na kuzitia kwenye gunia. Aliziuza na kuenda ulevini kwa Fiona kuwaburudisha walevi wenziwe. Haya yanajitokeza wazi alipokuwa akihojiwa na walevi wenzake alikozipata hela za kuwalevya ilhali amekuwa kwenye kituo cha polisi. Matari anakiri kwa kusema (uk 72)kuwa:-

Nilipotoka ndani nilipita kwenye makazi ya maaskari polisi.Nikaona nguo kadhaa zimeanikwanje.Wapuuzi hawa,wanaandika nguo nje, hawajui zinaweza kupeperushwa na upepo wa arijojo..........

Uk 72-73 anaendelea kusema:-

...............Nikaangalia mbele na nyuma hakuna mtu.Nikatazama kushoto na kulia,hamna mtu.Nitaangalia juu sikumwonaMungu na  chini sikumwona shetani.Nikaona gunia ......

Kwake Matari ulevi na wizi vimekuwa ngozi kiasi kwamba vimemwandama kama kupe kumbanduka si rahisi. Waaidha inathibitishwa wazi kuwa ana uhusianomkubwa sana katika kupoteakwa ng’ombe wa Tonge.Hii ilidhihirika wazi kupitia kutiwa nguvuni kwake ambapo Askari waliandamana na Jefule hadi kwa kina Matari na kumtia pingu kwa kushirikiana na Jefule kwenye huo wizi.

v  UASHERATI.

Hiki ni kitendo cha kupenda kuzini. Hali hii inadhihirika wazi kupitia wahusika mbalimbali katika tamthilia hii.Kwanza kabisa Fiona amejitokeza wazi kuwa kahaba wa Matari. Huyu ndiye mhisani wake wa uasherati. Hii ni kuwa uasherati wao huu umempelekea Matari kutumia mbinu zozote za kupalilia mwingiliano huo kwa kutumia hela za wizi. Matari ameonekana mara nyingi pindi anapoiba huelekea kiyuoni kwa kahaba wake muuza pombe Fiona. 

Mbali na Fiona, Vero pia amenaswa katika mtegohuowa Matari.Licha ya Vero kuwa shemegi yakeMatari, wawilihawa wanaingilia uasherati kiasi kwamba matendo yao yanasababisha uja uzito wa Vero.

Idara ya polisi pia imeathirika na uasherati. Kupitia kwa usemi wa Askari I ni ishara tosha kuwa hata yeye ni mwasherati mkubwa kwani anfikiria tu mwanamke upande wake ni wa mapenzi tu hakuna jingine la mno.

Askari I anasema  kuwa:-

........................... Nitapeleka salamu kwa dadako bila shaka kama yeye ni mzuri wa kugawa tenda na kufungasha vilivyo kama mwanamke halisi wa Kiafrika. Sivipendi visichana vya kisasa vinavyowaiga Wazungu na kujikondesha vikabaki kama shingo za flamingo.Namtaka mwanamke aliyeunga Sawasawa.....aliyekula akashiba......Nikipata nafasi nitamtafuta huyu dadako................

Isitoshe kupitia kwa mazungumzo kati ya MTU I na MTU II ni kuwa Lila ni changudoa tu mjini ila hakuna cha mno anachokifanya huko.

MTU II:Tena anavuta bangi, sikuambii kuvuta sigara. Fikiri mwanamke kuvuta sigara na bangi?Kajifanya kwenda mjini kufanya ajira ya usekritari kwenyeofisi ya mawakili sijui nini.Wapi bwana! Changudoa yule. Watu waliokwenda mjini wamemwona usiku akigombania waume.(uk 37) 

 

 

 

 

 

v  Hitimisho

Makala haya  yameangazia masuala ibuka katika Tamtilia ya Mbaya Wetu. Masuala ambayo yamejadiliwa ni :, mapenzi na ndoa, malezi, ufisadi,matumizi ya dawa za kulevya,Uasherati na ukiukaji wa haki za kibinadamu. Masuala haya yanatokea katika jamii tunamoishi. Hili linadhihirika kutokana na habari zinazoripotiwa katika vyombo vya habari kama vile magazeti.Visa vya ubaguzi wa wanawake vinashuhudiwa katika jamii.  Watu wengi huwaona wanawake kuwa viumbe ambao hawajakamilika wakupewa sikio katika maamuziya jamii.Wengine huwaona wanawake kuwa vyombo vya kuwaridhisha wanaume tu. Hii inatokana na dhana potovu kuwa mwanamke mahali pake ni jikoni tu. Mapenzi na ndoa ni suala linalochukua nafasi kubwa katika jamii yetu. Hii ni kwa sababu inajenga msingi wa familia na kuifunganisha jamii. Hata hivyo, asasi hii muhimu inakumbwa na changamoto tele zinazotokana na ukosefu wa mapenzi ya dhati. Tunashuhudia visa vya ukatili, ulevi, usaliti, uasherati, kutowajibika na talaka katika ndoa nyingi.

Suala la ufisadi ni janga katika mataifa mengi. Tunasoma magazetini kuhusu kashfa za ufisadi miongoni mwa viongozi kama vile: Goldernberg, Chickenigate na Angloleasing. Visa hivi vinatekelezwa na watui wenye tamaa na ubinafsi. Jamii  haitaki hawa kuwajibiki katika kazi zao na hawayajali maslahi ya wananchi wao huweka hongo. Hasa hili limepelekea kuzukakwa visa vingi vya uporaji mali ya umma kwa kuamini kuwa hongo ndiye mkombozi wao hasa kwenyeidara husika ambayo ni polisi. Hivyo basi ni ombi la kila mmoja kulivalia njuga swala hilina kuona kuwa maozo yote yanatiwa katika kaburi la sahau kwa kuwa pasi kufanya hayo jamii itazidi kuathirika pakubwa.

 

v  Marejeleo.

ü  Al Farsy, A. S. (1969) Kurani Tukufu. Nairobi: Paulines’ Publications Africa.

ü  Amulenga, C. M. na Amulenga, A. V. (2009) Solving Problems Occurring in Early
Marriages. Nairobi: Focus Publishers.

ü  Drabble, M. (1995) The Oxford Companion to English Literature. New York: Oxford University Presss.

ü  Farouk, M.T. (1974) Uchambuzi wa Maandishi ya Kiswahili. Nairobi: Oxford university press.

ü  Githinji, E. (2014) ‘Watoto Watatu Walioteswa Waokolewa’. Taifa Leo, Aprili 3, uk. 4

ü  Johnston, T. (2002) “Violence and Abuse of Women and Girls in Kenya, Population
Communication Africa. Nairobi: New World Printers.

ü  Kalama, M. (2013) ‘Mienendo ya Dada Zetu Yazidi Kukang’anya’. Taifa Leo, Juni 13, uk. 10

ü  Kamusi ya Karne ya 21 (2013). Nairobi: Longhorn Publishers Karanja, D. (2008) “Masuala Ibuka katika Fasihi ya Watoto’’. Tasnifu ya uzamili, Chuo kikuu cha Kenyatta.

ü  Kavuri, P. (2008) “Dhuluma za Watoto katika Riwaya za Kiswahili.” Tasnifu ya uzamili, Chuo Kikuu Cha Kenyatta.

ü  Kimani, C.W. (2003) “Swala la Dhuluma Dhidi ya Wanawake katika Fasihi Andishi ya
Kiswahili”. Tasnifu ya uzamili, Chuo kikuu cha Kenyatta.

ü  Masinjila, M. (1994) Teaching Oral Literature. Nairobi: Kenya Literature Oral Association.

ü  Njogu, K na Chimera, R. (1999) Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

ü  Onchong’a, E. (2013) ‘Malezi ya Wana ni Ushirika’. Taifa leo, Juni 17, uk. 11

ü  Shirika la AFP (2014) ‘Wamtetea Mfungwa’. Taifa Leo, Juni 20, uk. 13

ü  __________(2014) ‘Waziri Mkuu wa Zamani Ahukumiwa Miaka Sita Jela’. Taifa
Leo, Juni 24, uk. 13

ü  __________(2014) ‘Vita Vimeathiri Watoto Milioni Tano Syria’. Taifa Leo, Machi 12, uk. 13

ü  ___________(2014) ‘Wanahabari Waanza Mgomo Australia’. Taifa Leo, Mei 8, uk. 14

ü  __________(2015) ‘Albino Matatani’. Taifa Leo, Aprili 8 , uk. 13

ü  ___________(2015) ‘Kanisa Kupitisha Ndoa za Jinsia Moja’. Taifa Leo, Machi 19, uk. 13

ü  Walibora,K(2014) Mbaya wetu,Nairobi,Moran East Africa Publishers

 

No comments:

Post a Comment