Monday

Athari katika fasihi linganishi kisha kwa kutumia msingi huo, onyesha namna athari inavyojitokeza katika; Alfu Lela Ulela:Kitabu cha 1(Kisa cha walii Wa 11 na mbwa wawili weusi.

0 comments

 

Jadili kwa mapana Athari katika fasihi linganishi kisha kwa kutumia msingi huo,
onyesha namna athari inavyojitokeza katika; Alfu Lela Ulela:Kitabu cha 1(Kisa cha walii Wa 11 na mbwa wawili weusi.

Fasihi linganishi

Dhana ya Fasihi linganishi kwa kumrejelea Henry Remak (1971) anafasili fasihi linganishi kama uwanja wa kifasihi unaohusika na uchunguzi na mahusianao ya kifasihi nje ya mipaka ya nchi moja, pia kati ya fasihi na fani nyinginezo. Kwa maelezo haya ya Remak tunachoweza kusema ni kwamba fasihi linganishi haiishii kuangalia mahusino ya kifasihi peke yake bali huangalia mahusiano kati ya fasihi na fani nyinginezo zisizo za kifasihi.

 

 

 

 

Athari katia fasihi linganushi.

Fasihi linganishi imejengeka kwenye msingi kwamba fasihi zozote zinazopatikana katika ujirani mmoja hazina budi kuathiriana. Kazi za Muyaka Bin Haji zimeathiri kazi za washairi wa baadaye kama Juma Bhalo na Abdilatif Abdalla. Hata hivyo, athari za Muyaka hakuazimwa moja kwa moja na wafuasi wake. Kazi za watangulizi na wafuasi wanaopatikana katika ujirani mmoja zinaweza kulinganishwa na kulinganuliwa. Si hivyo tu; hata fasihi ambazo hazipatikani katika ujirani mmoja zinaweza kulinganishwa.

M.S. Abdullah na Conan Doyle wameandika masimulizi ya upelelezi. Abdulah anamfufua Sherlock Holmes, nguli anayepatikana katika masimulizi ya Conan Doyle na kumweka katika mazingira na muktadha wa Zanzibar. Isitoshe; Abdullah anakihamisha kipera cha masimulizi ya upelelezi kutoka Ulaya hadi Afrika Mashariki. Kazi za Abdullah na Doyle zinaweza kulinganishwa kwa msingi huo. Katika mkabala wa upelelezi kuna wandishi wengine wa kipelelezi kama John Simbamwene, Faraj Katalambulla na John Mtobwa wanaoweza kulinganishwa na kutofautishwa na mtangulizi wao, na vilevile wao kwa wao.

Aina za athari

Kiwewe cha kuathiriwa

Baadhi ya athari zinazowashughulisha walinganishi haziwezi kutambulika moja kwa moja. Huwa zimejificha na hutaka uzoefu mkubwa wa uhakiki ili zitambulike na kufichuliwa. Kwa hakika athari nyingine huwa kinyume na matarajio. Euphrase Kezilahabi ni mwanafunzi wa Shaaban Robert. Kezihalabi amelelewa kwa hekima ya shaaban. Amemsoma Shaaban na kuandika tahakiki nyingi juu ya Shaaban Robert zikiwemo Ushairi wa Shaaban na Riwaya za Shaaban Robert.

Hata hivyo katika ushairi wake na riwaya zake anaenda kinyume cha Shaaban Robert. Vilevile kila mwandishi huyu anaposoma riwaya za Clara Momanyi hasa Tumaini na Nakuruto pamoja na hadithi yake fupi, “Ngome ya Nafsi”, anakatikiwa kwamba kwa kiwango fulani, Momanyi aliathiriwa na Kezilahabi kwa njia ya kipekee. Aliathiriwa kwa kumkwepa na hata kumkosoa Euphrase Kezilahabi kwa mtazamo wake wa kukatiza tama juu ya mtoto wa kike. Mhakiki Harold Bloom ameandika tahakiki ya ushairi mashuhuri inayoitwa The Anxiety of Influence ambapo anadai kwamba mwandishi chipukizi anapotaka kuwa maarufu, lazima aepukane na sifa zilizomfanya mtangulizi wake kuwa mashuhuri na mtajika. Kezilahabi anakuwa mtajika kwa “kufadhaishwa” na athari za Shaaban Robert.

Naye Clara Momanyi anaendelea kupata umaarufu kwa kufaidhaishwa na athari za Euphrase Kezilahabi. Jambo hili linakutikana katika fasihi za Kimagharibi nyingi. Aristotle alikuwa mwanafunzi wa Plato. Wote walikuwa maarufu kwa njia tofauti kwa sababu Aristotle alikwepa mkondo wa kutafakari wa Plato ijapokuwa hakumkosoa mtangulizi wake moja kwa moja mtangulizi huyo akiwa hai. Katika bara la Afrika wandishi kama Ngugi wa Thiong’o na Chinua Achebe wameathiriwa na wandishi wa Kimagharibi kama Josef Conrad na W.B. Yeats mtawalia. Shujaa Okonkwo ni riwaya inayosomwa kwa sababu za kifasihi, kianthropolojia, kidini na hata kisiasa. Kazi kama hii inafaa sana kusomwa katika fasihi linganishi. Katika kitangulizi cha riwaya hiyo, mtunzi anaonyesha kinaganaga kwamba amesoma kazi za kishairi za mwanafasihi Yeats kutoka Ireland hasa shairi lake ‘The Second Coming’. Katika ‘The Second Coming’, Yeats anazungumzia matukio yanayosababisha kudidimia na kupomoroka kwa utamaduni na ustaarabu wa Kimagharibi. Ustaarabu anaouhofia ni ule uliojengeka kwenye misingi ya Ukristo, sayansi na teknolojia ya Kimagharibi. Kwake sayansi na teknolojia ya Kimgharibi ni kilele cha juu cha maendeleo ya mwanadamu. Ustaarabu huu unatishwa na ukafiri wa aina fulani.

Kiwewe cha kuathiriwa kinatokea pale ambapo Achebe anatumia taswira na vitushi vya Yeats ijapokuwa anayaweka malengo yake kichwamgomba. Ikiwa Yeats anatetea Ukristo na sayansi katika shairi lake, Achebe naye anatoa madai kwamba Ukristo, sayansi na teknolojia-zote asasi za mtu mweupe ndizo zimesababisha kudidimia, na kubomolewa kwa ustaarabu wa Mwafrika. Kile kinachotetewa katika shairi la Yeats kinageuzwa na kuwa kiashiria cha uovu na maangamizi katika jamii za Kiafrika. Harold Bloom aliishilia katika kuorodhesha hatua ambazo mtunzi chipukizi angezipitia ili apate umaarufu. Mwandishi huyu haamini kwamba lazima hatua hizo zote zipitiwe ili chipukizi apate umaarufu.

Mwingiliano matini

Mwingilianomatini ni dhana inayotumiwa kuezelea usemezano unaotokea kati ya sauti mbalimbali zinazopatikana katika matini. Sauti zilizopo kwenye matini wakati huu zinaweza kuwa mwangwi wa sauti za wakati uliopita, mwangwi wa sauti nyingine zilizopo na zitakazokuja baadaye. Mwingiliano matini ni kitengo cha usemezano ambayo kimsingi ni nadharia ya kiisimu jamii na fasihi. Katika isimu usemezano kwa mujibu wa maelezo ya Mikhail Bakhtin uwezo wa sajili mbalimbali kuingiliana na kusemezana kati yazo na vile kusemezana na misimbo ibuka kama msamiati mpya na vilugha vya vikoa tofautitofauti katika jamii. Dhana ya mwingiliano matini inaweza kuinuliwa kuwa kinadharia cha kuichangunulia fasihi linganishi. Mahali ambapo matini zinaingiliana patadhihirisha mshabaha mkubwa kati ya kazi za fasihi zinazolinganishwa.

Kinyume na haya mahali ambapo matini zitatengana sana kimaudhui na kimtindo patathibitisha tofauti zilizopo kati ya kazi za fasihi zinazohusika. Riwaya za Shaaban Robert kama Adili na Nduguze na Kusadikika zinaweza kulinganishwa na masimulizi ya Alfu Lela Ulela kwa misingi ya mwingiliano matini. Muundo na usawiri wa ni mambo yanayoingiliana hivi kwamba kuna uwezekano mkubwa kwamba kabla ya kuandika kazi zake Shaaban Robert alikuwa amedurusu masimulizi ya Alfu Lela Ulela. Mwangwi wa Alfu Lela Ulela unasikika katika kila hatua ya kusoma Adili na Nduguze na Kusadikika hususan tukizingatia Alfu Lela Ulela Kitabu cha Kwanza na Alfu Lela Ulela Kitabu cha Pili. Mwingiliano matini ni mkabala unaofaa wa kulinganisha na kulinganua kazi hizi. Riwaya ya Shaaban Robert ya Kusadikika inaweza kulinganishwa na riwaya ya Katama Mkangi ya Walenisi kwa kutumia mkakati huu pia. Ingawa masimulizi ya Alfu Lela yanaweza kulinganishwa na riwaya ya Walenisi, mshabaha hautalingana na tofauti. Kuna viwango mbalimbali vya mwingiliano matini ambavyo vinaweza kumsaidia mhakiki kujenga mihimili ya nadharia hiyo.

 

 

 

 

 

 

Athari katika Alfu Lela Ulela: Kitabu cha 1(Kisa cha walii Wa 11 na mbwa wawili weusi)

Katika hadithi hizi mbili, inadhihirika wazi kuwa athari ambayo imejitikeza moja kwa moja ni ile ya mwingiliano matini. Katika athari hii inabainika wazi kuwa miangwi ya kisa kimoja inatoa mirindimo katika kisa kingine ingawa mwandishi amejarubu kukwepa baadhi ya mifanyiko katika kila mojawapo wa visa hivi.

Kwenye kisa cha Walii wa Pili yapo mazingira ya safari inayopangiwa mwana wa Mfalme ambaye ameibuka gwiji wa elimu hasa dini na kuandika Kiarabu. Sifa zake hizi zilimfanya sultan wa Bara Hindi kumtuma mjumbe na zawazi ya utajiri kwa kumtaka mwanawe kuzuru kwa Mfalme wa Bara Hindi. Miangwi ya safari vile vile inajitokeza katika kisa cha Mzee wa pili na Mbwa Wawili Weusi. Hata hivyo safari hii ni ya tamaa za kibinafsi za Ndugu hawa wafanyibiashara kwenda pwani kufanya biashara. Kwa hivyo safari hapa licha ya ya kuwepo imepewa taswira tofauti.

Tukitazama kwenye rasilmali, inaonekana wazi kuwa kwenye kisa cha Mbwa wawili, hazina waliyo nayo hawa Ndugu wa watatu ni ya uridhi kutoka kwa baba yao ambaye kwa sasa ni marehemu. Kwenye kisa cha walii wawili tunamwona Mfalme akiyatoa mali yake kwa mwanawe ili ampelekee sultan wa Bara Hindi kama zawadi. Kwa hivyo swala la asili ya mali na hela za matumizi kwa wahusika hawa linajitokeza ingawa kwa ukinzani mkuu.

Swala la mikosi ya safari zote hizi mbili limeangaziwa. Kwenye kisa cha mbwa wawili weusi walendugu wawili waliotaka kauli ya kwenye kufanya shughuli zao za kibiashara waliporudi hahi zao kama zinavyoelezwa na ndugu yao, hazikufurahisha hata kidogo. Waliporudi walikuwa wanyonge na hali bin taabani na wamefilisika pakubwa ishara kuwa huenda walishambuliwa na wazi na kuporwa kila walichikuwa nacho. Kwenye kisa cha walii wawili, mikosi ya safari pia inajitokeza ambapo mtoto wa Mfalme na ujumbe wake walipokuwa safarini, waliweza kushambuliwa na wezi ambao walikuwa hamsini na kuwapora kila walichokuwa nacho licha ya kuwateka nyara wajumbe waliokuwa wakisafiri na mwanawe Mfalme. Kwa upande wake mwanawe Mfalme alipata kunusurika na kuhepana farasi wake ambaye alianga kutokana na Jeraha alililipata katika uvamizi ule. Mwanawe Mfalme kwaupande wake alijirusha nakuenda asikokufahamu mradi awe mbali na mikono ya wezi watekaji nyara wasio na utu asilani.

Kwenye kisa cha walii wa pili mwanawe Mfalme anapokea hisani kutoka kwa mshona viatu baada ya kutaabika msituni akila matunda ambapo anapata hifadhi, maakuli pamoja na zana za kujipatia riziki atakapokuwa katika nchi ile ngeni. Kwenye kisa cha mbwa wawili weusi vile vile waathiriwa wa awali ambao ni ndugu wawili wanapata hisani si kutoka kwa mtu wa mbali bali kutoka kwa ndugu yao ambaye aliwasihi wasiende kwenye shughuli zao za kibiashara ingawa wakadinda. Kila mmoja waoaliingia na maafa yake yaliyoandamana na kupunjwa kwa hela zao ikabidi ndugu yao awakirimu kwa kila kitu sawa na alivyokuwa mshona viatu na mtoto wa Mfalme.

Wale ndugu wawili waliweza kujifunza maswala yanayofungamana na biashara ambapo riziki yao ya kucha kutwa walijikimu kwa kutumia jasho lao la kibiashara. Tukitazama katika hadithi ya walii wa pili, mwanawe Mfalme hakuweza kujifunza walakufundishwa kazi yoyote ya kiufundi ya kujikimi maishani bali alitegemea tu wazazi wake. Hii ilidhihirika alipofika kwa mshona viatu ambaye alilazimika kumpa shoka na kumshauri kuwa mchaja kuni.

Visa vyote viwili vinaangazia swala la harusi katika mitazamo miwili tofauti kabisa. Kwenye kisa cha mbwa wawili weusi, harusi ni ya hiari ambayo Ilipendekezwa na jini kwenye umbo la binti mrembo. Harusi ile ilifungwa  na wawili hawa  wakaabiri chombo wakiwa na nia ya kurudi nyumbani kuishi kama mke na mume. Katika kisa cha walii wa pili, harusi iliyotarajiwa kati ya binti sultani wa Kisiwa cha Mpingo na bin Sultani aliyekuwa binamu yake, haikufaulu kwani binti aliwahiwa na jini la kiume ambalo lilimtia mateka na kumficha katika makaoyake hayo ya ajabu.

Wahusika hawa wote wawili wanapata hisani kutoka kwa wanawake wasiowafahamu kamwe. Kwenye kisa cha mbwa weusi wawili mhusika huyu ananusurishwa na jini mfanowa mwanamke wote wawili walipotupwa baharini ili wafe. Naye mhusika katika kisa cha walii wawili anapewa hisani kutoka kwa mwanake mateka wa jini ambaye anampamajiya kukoga, chakula na kumfariji kutokana na hali yake iliyokuwa ya kusikitisha ajabu.

Kisa cha Mzee wa Pili na Mbwa Wawili’, wanadamu wawili mbao walipanga njama ya kumwua ndugu yao pamoja na mkwewe ambaye alikuwa jini wanabadilishwa na hilo jini kama adhabu na  kuwa mbwa wawili weusi. Katika kisa cha walii wawili mhusika ambaye ni mwana wa Mfalme naye anabadilishwa katika kiumbe cha kupaa angani nakujikuta amerudi pale pale ardhini kwenye makao ya jini.

Ipo pia ile hali ya kubadilika kwa mazingira kijini kiasi kwamba binadamu wakawaida hawezi kutambua wala kubaini bayana. Kwenye kisa cha mbwa weusi, yule mtoto aliyenusurishwa na jini alijikuta kwenye paa lake la nyumba ilhali walirushwa baharini. Kwenye kisa cha walii wawili tunaiona hali kama hiyo ambapo jini lajigeuza binadamu na kumjia mtoto wa sultani na kumtwaa kwa hali isiyoeleweka na kujikuta kwenye makao ya jini.

Katika kisa cha mbwa wawili weusi halikukubali yule binadamu aangamie walipotupwa baharini hivyo likamwokoa kwa hali isiyoeleweka na mwanadamu wa kawaida. Katika kisa cha walii wawili hapa mwanadamu ambaye nimkewe jini anamwokoa mtoto wa sultani katika haili ya kawaida kwa kukataa kumwangamiza kwa silaha aliyopewa na jini kwa kusema kusema kuwa hakuwa na nguvu za kushika upanga.

Mwingiliano uliopo kwenye visa hivi viwili vile vile unaonekana kupitia kwa wahusika. Katika kisa cha mbwa wawili weusi mwanamke anayemrai binadamu kumwoa ni jini na hili linadhihirika wakati ambapo linamwokoa atupwapo baharini. Katika kisa cha walii wawili nacho mwanamke anayemwokoa mtoto wa sultani si jini bali ni binadamu wa kawaida aliyekuwa ametekwa nyara na jini.    

Hitimisho

Kwa yakini fasihi linganishi hasa athari ya mwingiliano matini imejitokeza waziwazi katika visa hivi viwili kiasi kwamba mwandishi amekitumia kisa kimoja kukijenga na kukikamilisha kisa kingine. Hata hivyo inaonekana kuwa kwenye kisa cha mbwa wawili weusi mazingira ya kimwambao yanajitokeza dhahiri na kwenye kisa cha walii wawili mazingaira hayana msabaha wowote na upwa. Wahusika nao vile vile wameingiliana kwa njia moja hadi nyingine kulina na majukumu wanayoyatekeleza kwenye visa hivi viwili.

 

 

 

Marejeleo.

Abdalla, Abdilatif (1973). Sauti ya Dhiki. Nairobi: Oxford.               

Achebe, Chinua (1965). Morning Yet on Creation Day. London: Heinemann

Althuser, Louis (1981). Ideology and Ideological Apparatuses, Lenin and Other Essays

            London: New Left Books

Aristotle (1984 ) The Rhetoric. Trans. W. Rhys Roberts. New York: Dover Publications.

Press

Bakhtin, Mikhail (1981). The Dialogic Imagination. Austin: University of Texas Press.

Bakhtin, Mikhail (1984). Problems in Dostoevsky’s Poetics. Manchester: Manchester            University Press.

Bakhtin, Mikhail (1986). Speech Genres and Other Late Essays. Austin: University of          Texas Press

 Dan, Ben-Amos (1977). Folklore Genres. Bloomington: Indiana University Press

Bloom, Harold (1973) The Anxiety of Influence. New York: Oxford University Press.

Gifford, Henry (1969). Comparative Literature: Concepts in Literature. London:      Routledge & Paul Kegan

Habwe, John (2008). Cheche za Moto. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Harries, Lyndon (1962). Swahili Poetry. Oxford: Clarendon Press.

Hichens, William (1972). Al Inkishafi. Nairobi: Oxford University Press.

Kareithi, Peter  (1969) Kaburi Bila Msalaba. Nairobi: East African Publishing house.

Kezilahabi, Euphrase (1971). Rosa Mistika. Nairobi: Kenya Literature Bureau.

King’ei, Kitula (2007). ‘Athari za Washairi Wakongwe juu ya Washairi wa Kisasa:

Mfano wa Muyaka Bin Haji na Ahmad Nassir’ Kioo Cha Lugha. vol 5 (30-38). Dar es Salaam: Idara ya Kiswahili.

Lukacs, Georg (1962). The Historical Novel. Lincoln: Nebraska University Press.

Mkangi, Katama (1995). Walenisi. Nairobi: East African Educational Publishers

Mkangi Katama (1984). Mafuta. Nairobi: East African Educational Publishers.

Mlamali, Hamad (1980). Inkshafi: Ikisiri. London: Longman.

Mohamed, Suleiman (1976). Nyota ya Rehema. Nairobi: Oxford.

Mohamed, Said Ahmed ( 2001). Babu Alipofufuka. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation

Mohamed, Said Ahmed (1980). Dunia Mti Mkavu. Nairobi: Longman

Momanyi, C. Tumaini. Nairobi:  Vide~Muwa Publishers Limited, 2006.

Mulokozi, Mugyabuso (1979). Mukwava wa Uhehe. Nairobi: East African Publishing           House

Ngare, J (1974). Kikulacho ki Nguoni Mwako. Nairobi: East African Publishing House.

Orwell, George (1967) Shamba la Wanyama. Taf. ya Kawegere. Nairobi: East African

            Publishing House

Shafi, Adam (1978). Kasri ya Mwinyi Fuad. Dar es Salaam : Tanzania Publishing House.

Sofokile, (1969) Mfalme Edipode. Nairobi: Oxford

 

Valdes, Mario et al (1992). Comparative Literature as Discourse. Bern: Berlin: Peter            Lang

Wafula, Richard Makhanu (1999) Uhakiki wa Tamthilia: Historia na Maendeleo Yake.

            Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation

 

No comments:

Post a Comment