Monday

uhakiki wa maudhui katika Mimba ingali mimba na hadithi nyingine

0 comments

HAKIKI MAUDHUI YANAYOJITOKEZA KATIKA MIMBA INGALI MIMBA NA HADITHI NYINGINE (MC ONYANGO,2006).

Maana ya Maudhui

Kwa upande wa maudhui imekuwepo mikinzani na mikanganyiko nuongoni mwa wanataaluma wa kazi za fasihi juu ya maana yake. Wengi wa wananadharia hao wanajadili fani na maudhui pamoja, japo pengine mitazamo yao haiwi sahihi.

Baadhi ya wanataaluma wa kazi za fasihi wanasema kwamba fani na maudhui ni vipengele ambavyo havina uhusiano wowote na kwamba vinaweza vikatenganishwa. F.V. Nkwera analinganisha fani na maudhui na kikombe na maji. Kikombe kinachukuliwa kama ndiyo fani, na upande mwingine maji ndiyo maudhui. Mnywaji wa maji hayo analinganishwa na msomaji wa kazi ya fasihi.

S.D.Kiango na T.S.Y.Sengo  wanafafanua fani na maudhui kwa kulinganishwa na chungwa ambalo lina sehemu ya nje na ndani. Maudhui ya kazi ya sanaa yanalinganishwa na nyamanyama za chungwa na fani ni ile sehemu ya nje.

Mawazo mengine juu ya fani na maudhui yanatolewa na Penina Muhando na Ndyanao Balisidya ambao wanaelekea nao kuukubali mtazamo huu ulioelezwa hapo juu wakati wanapoelezea hadithi kuwa na "umbo la nje" wakati lugha inapotumiwa na kujenga hilo umbo la ndani (maudhui) ambalo huhusika na wazo kuu analolitaka fanani, (dhamira) ujumbe wake, maadili, na falsafa zake (kama zipo) za maisha."

Nadharia hizo zote zilizojadiliwa hapo juu kwa ujumla zinaonyesha kupwaya na zinaweza kuwakanganya wasomaji. Nadharia hizo hazionyeshi ama kuwakilisha ukweli wa mambo ulivyt) juu ya uwiano uliopo kati ya fani na maudhui katika kazi ya sanaa kwani zinaonyesha kuwa fani na maudhui ni vitu viwili vinavyoweza kutazamwa katika utengano, jambo ambalo si la kweli. Ukweli ni kwamba vitu hivi viwili vinategemeana na kukamilishana, na wala havitazamwi katika utengano.

Ufafanuzi wa kuiona fani na maudhui kama kitu kisichoweza kutenganishwa umefanywa na Henri Arvon, Avner Zis na wanataaluma wengine wengi walio na mtazamo wa kisayansi ama kiyakinifu.

Kwa upande wa fasihi ya Kiswahili, M.M. Mulokozi na K.K. Kahigi wamekuwa na mtazamo wa aina hiyo pia. Wanafasihi hao wanasisitiza kuwa "fani na maudhui huathiriana na kutegemeana ... Maudbui ni maana ya shairi (kazi ya sanaa), ni yale mawazo yanayozungumzwa (dhamira, falsafa, maoni), pamoja na mtazamo wa mtunzi juu ya mawazo hayo... wazo kuu (dhamira) na mtazamo wa msanii hutupa ujumbe."

Akiungana na mtazamo huu, Senkoro naye anasema kuwa "maudhui ni jumla ya mawazo, mafunzo yapatikanayo katika kazi ya fasihi... Maudhui huunda lengo kwa mwaudishi. Kutokana na lengo, mawazo na mafunzo ya mwandishi ndipo tunapata falsafa. Mawazo, mafunzo, lengo na falsafa au mtazamo wa mwandishi kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii huunda msimamo."

Mawazo hayo aghalabu yanajaribu kufafanua nini hasa ni maudhui. Lakini dhana ya kutotenganishwa kwa vitu hivi viwili haijawekwa waziwazi. Ndipo Senkoro anapotumia mfano wa "sarafu" kwa kufananisha fani na maudhui ya kazi ya sanaa na "sura mbili za sarafu moja." Mfano huu unajaribu kusisitiza dhana ya kutotenganishwa kwa fani na maudhui katika kazi za sanaa za kifasihi. Mfano huu wa sarafu unajaribu kuonyesha dhana ya ukamilifu ya fani na maudhui kama kitu kimoja cha kazi ya sanaa kwa kutumia mfano wa sarafu yenye sura mbili, lakini umuhimu wake kama sarafu moja unategemea tuweko kwa sura hizo mbili. Sura moja ya sarafu ikikosekana, basi, sarafu hiyo haiwezi kuwa na hadhi yake ya kisarafu. Jambo la muhimu ni kuona jinsi kitu kimoja (fani) kinavyoweza kukikamilisha kingine (maudhui).

Kwa kuzingatia nadharia hizo, tunakubaliana na Senkoro  au Mulokozi na Kahigi  wanaosema kuwa "fani na maudhui huwiana, hutegemeana na hatimaye kuathiriana." Uhusiano huu ndio unaojenga kazi bora ya fasihi. Aidha ni vizuri kutoa tahadhari hapa kuwa uwiano wa fani na maudhui wa kazi ya sanaa huwa ni lengo la msanii. Maudhui iliyotawala kuumbwa kwa kazi ya sanaa inatakiwa kujitokeza katika fani inayohusu. Ili maudhui yatawale fani, sharti yajitokeze kama kazi ya sanaa na si kama hotuba ya mwanasiasa. Ni wajibu wa msanii kuchagua fani inayomruhusu kutumia maudhui anayotaka kuyafikisha kwa hadhira yake.

Vipengele vya maudhui ni pamoja na dhamira, migogoro, falsafa ujumbe na msimamo.

1.   Dhamira; hili ni wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika kazi ya fasihi. Dhamira ni sehemu tu ya maudhui na aghalabu dhamira kuu ndio hujenga kiini cha kazi ya fasihi. Dhamira zimegawanyika katika makundi mawili, kuna dhamira kuu na dhamira ndogondogo.

2.   Migogoro; hii ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi za fasihi. Migogoro inaweza kuwa kati ya wahusika, familia zao, matabaka yao, au hata katika nyadhifa mbalimbali. Vilevile migogoro yaweza kuwa ya kiuchumi, kijamii, mogogoro ya nafsi, na migogoro ya kisiasa ambayo hujitokeza katika mitazamo tofauti kulingana na mtiririko wa visa na matukio yanavyopangwa na mwandishi.

3.   Ujumbe; mwandishi anapoandika kazi yake huwa na ujumbe ambao hutaka uifikie jamii aliyoikusudia. Ujumbe katika kazi fasihi ni mafunzo mbalimbali ambayo hupatikana baada ya kusoma kazi ya fasihi. Katika kazi ya fasihi dhamira kuu hubeba ujumbe wa msingi na dhamira ndogondogo hubeba ujumbe ambao husaidia kuujenga au kuupa uzito zaidi ujumbe wa msingi.

4.   Msimamo; katika kazi ya fasihi, mawazo, mafunzo na falsafa ya msanii hubainisha msimamo wake kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii. Msimamo ni ile hali ya mwandishi kuamua kufuata na kushikilia jambo fulani. Jambo hili huweza kukataliwa na wengi lakini akalishikilia tu. Msimamo ndio huweza kuwatofautisha wasanii wawili au zaidi wanaoandika kuhusu mazingira yanayofanana. Kwa mfano, katika tamthilia ya “Pesa zako zinanuka” mwandishi anamsimamo wa kimapinduzi kwani amejadili matatizo yanayochangia kukwama kwa ujenzi wa jamii mpya.

5.   Falsafa ni mawazo ya busara yenye kutawaliwa na misingi mahususi juu ya asili na maana ya ulimwengu na maisha ya mwanadamu. Ni msimamo wa msanii katika maisha juu ya utatuzi wa matatizo katika jamii. Falsafa ya mwandishi inaweza kujulikana kwa kusoma kazi zake zaidi ya moja.

6.   Mtazamo ni hisia au uelewa wa mwandishi juu ya jambo fulani. Kwa mfano anaweza kutazama jambo fulani kwa mtazamo wa kidini, au anaweza kutazama jambo fulani kwa mtazamo wa kisiasa au kisayansi.

7.   Mafunzo; ni mawazo ya kuelimisha yanayopatikana katika dhamira mbalimbali za kazi ya fasihi.

Uhakiki wa Maudhui katika Mimba ingali mimba na Hadithi Nyingine

KJwa kweli huu ni mkusanyiko wa hadithi ambazo moja kwa moja zinaiafiki jamii ya sasa. Mhariri ameziteua hadithi hizi kwa ustadi ili kulitimiza lengo lake katika jamii. Maudhui haya yamejiratibu ifuatavyo kutoka hadithi moja hadi nyingine.

Bimdogo Selina

Elimu

Maudhui ya Elimu yamejitokeza wazi wazi katika hadithi hii. Tunakumbana na Selina ambaye anaishi na Shangazi yake kwa jina Shefsa. Hali ya masomo ya Selina inaingia mchanga kwani hapewi mazingira mazuri ya kumwezesha kusoma akiwa na Utulivu.

Selina huamshwa asubui na mapema akakoga na kuondoshwa halahala kabla hata ya kuimaliza chai yake ili aende shuleni kwa kupitia sehemu fulani za kisiri ambazo yeye mwenyewe hakuweza kufahamu mzigo aliokuwa akipewa kumpelekea Kionyeshaa kila asubui.

Sare yake ya shule haitamanishi pamoja na vyatu vyake ambavyo hali yake inatia hofu na mashaka.

Kwa kweli elimu kwa mtoto wa kike bado ni changamoto kiasi katika baadhi ya jamii zetu za Kiafrika. Hii ni kutokana na mila ambazo zimepitwa na wakati pamoja na taasubi za kiume kuwa mwanamke hafai kwa lolote wala chochote.

Matumizi ya Mihadarati- dawa za kulevya

Kila asubui Selina anaoondoka kwenda shuleni, Shangazi yake alikuwa akimpa kijimzigo kidogo kukifikisha kwa Kionyeshaa. Mwanzoni hakufahamu hadi alipotiwa mbaroni na polisi walienda Usalama. Tunazidi kuona namna jamii kwa kupitia wateja wake Kionyeshaa inavyoathirika na matumizi ya mihadarati.

Dhuluma kwa watoto wa kike.

Kupitia kwa maisha ya Srlina na Shangazi yake, inadhihirika wazi kuwa mtoto wa kike anakumbwa na vizuizi vingi mno katika maisha yake. Wanapewa majukumu hatari yanayoweza kuwatika Mashakani na hatarini.Kwa mfano Selina alikuwa akitimiwa katika usafirishaji wa dawa za kulevya kutoka kwao nyumbani hadi kwa Kionyeshaa. Licha ya kutumiwa kama mrija wa kitega-uchumi, Shangazi yake hamshughulikii katika maswala  ya kimsingi kama Mavazi, chakula n,k..

Mimi Sijui

Uramali/Uganga/Usihiri

Katika jamii husika inathibitika wazi kuwa watu wanathamini sana Mazingaombwe kuliko maswala halisi.Hii inathibitika wakati wakazi hawa wamesusia kutazama mechi ya mpira uwanjani ili waweze kutazama Mazingaombwe yanavyoendelezwa. Wanastajabia mabadiliko ya vitu asilia kutoa vitu vingine kabisa.

Ulevi

Maudhui haya yanajitokeza kupitia kwa mhusika Hamsini Zangu ambayo daima yuko mbioni kutafuta mteja wa kukinunua alichonacho ili apate hela za kununua kileo. Baada ya muda mfupi, bwana huyu anatokeza akiwa mlevi chakari hajijui hajitambui.

Uchachu huja Baadaye

Elimu

Hii ni hadithi ambayo Waaidha imeangazia swala la elimu. Tunakumbana na wahusika mbalimbali wakiwa katika mazingira ya elimu. Hawa ni pamoja na Moronya na Kimbo. Wawili hawa wako katika awamu ya mwisho katika chuo ambapo wanasomea utabibu.

 

 

Ukengeushi

Hali hii imedhihirika kwa wahusika mbalimbali ambao kinyume na lengo lao masomoni, hujkubali kunaswa na ufuska fulani. Baadhi ya wahusika hawa ni pamoja na Moronya ambaye amewajaza wasichana kwenye mwili kama Mavazi huku wakipokezana zamu katika chumba chake cha malazi.

Ufuska huu haukukomea hapo chuoni bali hata baada ya kudarijiwa na akaanzisha zahanati ndogo mjini Nakuru na rafiki yake, tunamwona akizidi tu kuzama katika Usherati kwa kuwavizia wake za watu ambao huja kwake roho safi wakihitaji huduma za kiafya. Vitendo vyake hivi ndivyo vilivyomwingiza kaburini huku akiwa na majuto chungu nzima.

Ukimwi

HIV (VVU) ni mdudu mdogo sana, inajulikana ka virusi, kwamba huwezi kuona. UKIMWI (Upungufu wa Kinga Mwilini) ni ugonjwa ambao unaendelea baadaye, baada ya mtu kuambukizwawa virusi vya UKIMWI. 



Mtu hupata UKIMWI wakati mfumo wa kinga unapokuwa dhaifu na kushindwa kupigana na maambukizi. Mara nyingi dalili ni; Kuwa mgonjwa kwa muda mrefu na magaonjwa ya kawaida kama vile kuhara au mafua. Dalili za UKIMWI zinaweza kuwa tofauti kutoka kwa mtu mwingine hadi mwingine. Mtu aliye na UKIMWI anaweza kupata maambukizi ya magonjwa amabayo huwa nadra kwa wasio na virusi vya ukimwi, kama baadhi ya saratani au maambukizi ya ubongo. 

Lishe bora na madawa yaweza kusaidia mwili kupambana na maambukizi na kukumuwezesha kuishi kwa muda mrefu. Lakini hakuna tiba ya virusi vya ukimwi. 

Janga hili limekuwa tisho kubwa katika jamii zetu. Watu hufa kucha kutwa bila hodi wala karibu. Hapo tunakumbana na Moronya ambaye tabia zake za Uasherati zinamsababishia gonjwa la ukimwi ambalo linamwanamiza. Hali yake hii inaweza kuafiki methali, “ Mwanamaji wa kwale kufa maji mazoea”

 

Majuto 

Maudhui haya yanajitokea kwenye wahusika mbalimbali. Mkewe Moronya anabaki pweke katika bahari ya majito kuhusu kifo cha mumewe akikosa kujua namna ya kuijenga na kuiendeleza jamii. Kwa upande mwingine, Moronya naye anajutia matendo yake ya ufuska anapokuwa katika hali zake za mwisho duniani. Wazazi wake Moronya nao hawakusazwa. Hawa walikuwa na ndoto ya kupata mtoto ambaye angekuwa tabibu ili kuiokoa jamii. Maombi yao hayakuwa na chochote wala lolote walipogundua kuwa mwanao alikuwa ameambukizwa maradhi ya ukimwi na hali yake ilikuwa taabani ambapo mauti yalimkodolea macho.

Jeraha la Raha

Uasherati

shannie na Dabbo ni makahaba ambao wanajiuza na wakinaswa wanatumia ngono na polisi kama malipo ya kuwawacha wenzao walioshikwa huru ale polisi waotawaliwa na kasumba hii wanadhihirika kupitia kwa inspekta Karama.Ulafi wa kimapenzi wa Karama ndio unaomletea fedheha.

Mihadarati

Shannie anajitokeza kama mtumizi hodari na hatari wa dawa za kulevya. Hii inadhihirika wazi anapowawacha Dabbo na Mnaziri katika hoteli ya Beach View Kunduchi, anaenda kwake kupanga mikakati ya kazi yake        . Tunamwona Shannie akimhadaa Karama ili wakutane kwa mahaba kumbe ulikuwa ni mpango wa kumtia dawa za kulevya ili Karama aabike kupita kiasi. Hili Shannie alilitekelezeakatika chumba na,bari 28 kwenye hoteli ya kimataifa ya Sea line ambayo ipo ufukweni mwa Bahari ya Hindi eneo la Oysterbay.

Kisasi

Shannie anapanga kisasi kwa Karama kwa swala la kuwadhulumu kimapenzi wanawake ambao waume zao walikuwa wameitwa mbaroni. Hili alilitekeleza kwa wepesi sana kutokana na tamaa ya kimapenzi aliyonayo Inspekta Karama.Alilitekeleza hili kwa wepesi mno na hakupatikana popote na wale wote walikuwa washukiwa, waliachiliwa kwa kukosa ushahidi wa kutosha. Shannie kwa upande wake akabaki salama wa salmin.

Unafiki

Inspekta Karama anatiwa shimiri na Shannie na kumfanya Karama kutenda kwa kazi yake na wenzake kule Morogoro kufanya uchunguzi kuhusu mauaji yaliyotokea katika eneo la Msamvu. Alipiga bongo na Shannie ili awadanganye wenzake kuwa ameshikwa na Ugonjwa wa ajabu wa kuanguka maruhani. Hii ilikuwa tu mbinu ya kupata muda mwafaka wa kukutana kimapenzi na Shannie pasi kujua yaliyomngoja mbeleni.   

Siri ya Mama

Ustahaimilivu

Maulidi alivumilia kukaa na (Rehema) mkewe kwa muda wa miaka minane bila ishara yoyote ya kupata mtoto.

Rehema alivumilia tabia za Maulidi kulala nje kwa mkewe mpya mtakiwa bila kuteta hata siku moja.

Ukewenza

Mke mpya kutaka Maulidi amwache mkewe wa kwanza kwa kuwa alionekana kuwa tasa.

Mke wa pili kumshauri wa tatu kuimba wimbo wa kuachwa kwa mke wa kwanza.

Tamaa

Maulidi kutamani kuwa na watoto kutoka kwa Rehema

Rehema kutamani mumewe akubali kupimwa

Maulidi kuzidi kuwa na tamaa ya mtoto wa kiume baada ya mkewe wa pili kudinda kuzaa tena baada ya kumzalia watoto watatu wote wasichana.

Umdhanaye ndiye kumbe siye.

Maulidi ndiye aliyekuwa na matatizo ya kizazi kinyume na alivyojijua.

Rafiki yake Maulidi kumpa ushauri ambao hauna msingi wowote.

Rehema kudhaniwa tasa kumbe la.

Mke wa pili kudhaniwa kuwa mwaminifu kumbe ni mcheza kando.

Siri

Wale wanawake wa pili na wa tatu wanafanya siri ya kuwazaa watoto nje ya ndoa huku wakimdanganya Maulidi kuwa yeye ndiye baba halisi wa watoto wanaozaliwa.

Rehema anaakubali kuiweka siri ya hali halisi ya Maulidi hata baada ya kufichuka kuwa Maulidi ndiye aliyekuwa na matatizo ya kizazi ambapo risasi alizizitoa hazikuweza kuua.

Siri ya hali ya kasoro ya  Maulidi yafichuka alipokubali kupimwa ili kuthibitisha ukweli halisi ulipokuwa.

Sitaki

Usaliti

Franklin anasaliti uhusiano wake na kimwana ambaye alimhadaa hapo awali-Nyamweko.

Uraibu

Wawili hawa walikuwa waraibu wakubwa wa kupiga mtindi katika mwanzo wa uhusiano wao hali ambayo Nyamweko anailalamikia wakati wanapokosana. Anasema kuwa kila mara waliporudi usiku wakiwa walevi jambo ambalo liliwaudhi wazazi wa Nyamweko.Uraibu huu ulijumlisha ufanyaji wa mapenzi kiholela ambapo Nyamweko aliweza kupata uja uzito ambao Franklin alimkana kwa kinya kipana.

Mjuto

Vijana wanaojiingiza katika mapenzi ya mapema hujikuta wakijutia uamuzi wao huo. Nyamweko anajutia natendo yake ya kuwadharau wazazi wake kwa kufumbwa macho na mahaba kati yake na Franklin.

Uchungu wa mwana

Mamaye Nyakwemo alimtetea kila mara aliporudi nyumbani akiwa mlevi na Franklin hali ambayo ilimsababishia kichapo kutoka kwa babaye Nyakwemo.

Alipofukuzwa kwa mpenzi wake, alikaribishwa na mamaye ambaye alimsamehe kisha kumpa vifungu vya Bibilia kama kumpa moyo na imani. Alichukua fursa vile vile ya kumwombea msamaha kwa babake.

Uasherati

Vijana wa kiume wakiwakilishwa na kina Franklin, wanajiingiza katika maswala ya usherari ambapo wanakuwa na tabia za kuwaringa mimba wasichana wasiokuwa na ufahamu wa kimaisha. Pindi wanapowatinga mimba, hawawajibiki kwa lolote huku wakiwakashifu wahusika kuwa malaya.

Matendo maovu ya vijana hawa yanashinikizwa na wazazi wao hasa baba zao ambao wanawapa vichwa vigumu vya kuzikana mimba hizi pindi zinapotokea. Hawaonekani kuwajibikia matendo yai maovu bali wanawawachia wasichana hawa kujishughulikia wenyewe kabisa.

 

Mimba Ingali Mimba

Tamaa na matumaini

Nekesa alikuwa na tamaa na matumaini  ya  kuitwa mzazi ingawa kila kuchao hali hubakia vile vile. Tamaa yake hii inabaki kitendawili kwani hadithi inapokamilika hali yake inabaki vivyo hivyo akisubiri heri ambayo haijui itakapofika.

Mila na tamaduni

Katika hali yake ya uja uzito,alijikuta akisghulikiwa kadri jamii ilivyotaka hasa wakati mwanamke awapo na uja uzito.

Waliohujumu ujamaa

 

 

Mauti/Mauko

Hadithi inaanza na kifo cha Fisi ambaye alikuwa Ndugu yake ingawa hakikuwa kifo kamili bali mtego tu wa kutimiza kiu chake cha kula nyama za wenziwe.

Uroho

Binadamu kurithi na kumiliki takribani kila kitu huku viumbe wengine wakitaabika kwa kukosa riziki.

Ananyemelea mbuga la wanyama, kukatwa kwa miti kwa wingi.

Kusababisha kukauka kwa vyanzo vya maji vilivyosababisha mito kukauka.

Ujamaa

Wanyama kukusanyika katika kuomboleza kifo cha fisi. Kumboleza kwa mtindo kipekee na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu.Ngri kuongoza shughuli za mazishi.

Fisi kuijenga nyumba kubwa akiwana lengo la jamaa zake kupata mahali pa kupumzikia na kulala wanapomtembelea.Hakutaka wengine kulazimika kukaa nje kwa ukosefu wa nafasi.

Ulafi

Inadhihirika wazi kuwa Fisi kama anavyojilikana kuwa mlafi, alijijengea nyumba yake kubwa kama kisingizio cha udugu na ujamaa kumbe alikuwa na mpango wake fiche. Hii iligunduliwa na Sungura mbaye ni kakake alipokuwa akiuchungunguza ule mwili wa Fisi na kukosa kuona ukiwa wa mfu bali umelazwa kwa silaha kali. Walipokuwa katika maombolezo kamili, Fisi alitokeza na kuwaua wale wanyama wote kwa kutumia vifaa alivyokuwa amevilalia.

 

 

Mji wa New York

Ubaguzi

Hili linajitokeza katika hotuba iliyotolewa na Adu Emeka katika ukumbi wa mikutano kwenye Umoja wa Mataifa. Hotuba yake ilionyesha kupinga vikali namna visa vya ubaguzi vilivyotanda katika nchi mbalimbali zikiwemo Mashariki ya kati, Zimbabwe, Namibia na Afrika Kusini ambako ubaguzi wa rangi ulikuwa umekita mizizi. Wamarekani halisi hawawatambui Wamarekani weusi ingawa hao weusi ndio walioshika uchumi wa taifa hilo.

Unafiki

Licha ya Wamarekani kujifanya wanapinga ubaguzi wa rangi kule Afrika Kusini ilhali hawakuwa wakifikiria unyama wao nyumbani wa kuwanyanyasa na kuwabagua Wamarekani wenye ngozi nyeusi.

Uhayawani

Yule bwana aliyekuwa amevalia suti yenye manyoya ya kondoo alijifanya kuwa mwelekezi wa balozi kumbe ni mhalifu na mnyang’anyi mkubwa. Alimpiga balozi kabari na kumwonya kuwa iwapo angepiga ukelele basi angekiona cha mtema kuni.

Alimnyang’anya balozi kila senti aliyokuwa nayo akitishia kumwua.

Licha ya kuibiwa hela zake Balozi anapofika kwenye kituo cha kukatia tiketi ya gari , yule mkata tiketi hakuta kumsikiza hata kidogo na kumjibu kwa ujeuri kabisa.

Visa vya utekaji nyara na mauaji kiholela vimetanda katika mji wa New York kiasi kwamba hata wengine ambao ni wamerika huwaua watu kama njia moja ya kujifurahisha.

 

 

Usherati

Ni imani ya wakazi wa eneo atokako Balozi kuwa vifo vingi vya wanaume huwa mikononi mwa wanawake. Hii ni kwa sababu wakati balozi anapokuwa taabani, mwandishi anasema kuwa watu wa kwao wangeamini kuwa alikufia mikononi mwa mwanamke fulani.

Kasheshe jijini

Mauti/Maangamizi

Mlipuko wabomu ambao uliwaacha wengi wakiwa hoi katika bomu lilitegwa kwenye ubalozi wa Merikani jijini Nairobi Waliobaki kwenye matatu aliyosafiria msimulizi waliangamia kwa kuwa msimulizi anasema kuwa aliiona matatu ile ikiteketea.Watu wengi waliweza kuaga dunia akiwemo mhusika Rose.

Ujamaa na udugu

Wananchi walijitolea kuwasaidia waathiriwa wa mkasa huo wa bomu pamoja na vikosi mbalimbali vya Wanajeshi vilivyowasili ili kufanya uchunguzi pamoja na kuwaokoa waliokuwa wamekwama kwenye vifusi vya jingo hilo.

Mganga wa Tanga

Kutowajibika

Mamaye Dalo alimsubiri Daktari wa mchana kutoka alipoenda kupata kishuka bila ufanisi wowote. Daktari yule hakurudi kamwe. Ilipofika usiku takriban saa moja na nusu ndipo Daktari wa usiku alipofika.

Uganga

Jamii ya kina Dalo umeamini sana katika swala zima la uchawi. Hii inatokana na imani kuwa ni mganga tu ambaye angeweza kumtibu mtoto wao kutokana na Ugonjwa wake wa ajabu.

 

Kisasi

Jamii ya kijana aliyeiawawa na Dalo walipososana kwenye pilkapilka zao, alifanya Mazingaombwe ya kimila ili kuhakikisha kuwa wanalipiza kisasi.

Tamati

Hadithi katika kitabu cha hadithi fupi zinaingiliana moja kwa mojakatika maudhui. Hali hii inajitokeza waziwazi kwanzia kwenye hadithi tangulizi hadi tamatisha. Imejitokeza wazi kuwa maswala ibuka katika jamii za kisasa kama matumizi ya mihadarati, unyanyasaji wa mtoto wa kike , mila na tamaduni zilizopitwa na wakati, taasubi ya kiume,ujamaa na udugu yamejiweka wazi.

Kupitia kwa haya, waandishi hawa walikuwa na nia na madhumuni ya kuipa mwangaza jamii kuhusu hali halisi ya maisha na namna ya kulikabili hali hiyo.

Marejeleo

a.     Njogu, K. & Chimerah, R  (1999):  Ufundihsaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu.Nairobi: Jomo  Kenyatta foundation.

b.     Mohamed,S.A. (1995):  Kunga za Nathari ya Kiswahili.  Nairobi:  Oxford

c.      University Press.

d.     Wamitila,K.W. (2002):  Uhakiki wa Fasihi: Misingi na Vipengele Vyake.  Nairobi:Phoenix Publishers Ltd.

e.     Balisidya, M.L. (1987): ‘Tanzu na Fani za Fasihi simulizi’ katika MulikaNa 16. Dar es Salaam:  T.U.K.I.

f.       Njogu, K.   & Chimerah, R.   (1999): Ufundishaji wa Fasihi:   Nadharia na

g.     Mbinu Nairobi: J.K.F.

h.     Mazrui, A.M. & Syambo, B.K. (1992):  Uchambuzi wa Fasihi. Nairobi:

E.A.E.P.

i.        Sengo,T.S.Y.  (1987):Fasihi  Simulizi:  Sekondari  na  Vyuo  Dar-es Salaam Nyanza Publications Agency.

j.       MCOnyango, O(Mh)-2008: Mimba Ingali Mimba na hadithi nyingine. Nairobi,Focus Publishers Ltd

 

No comments:

Post a Comment