Monday

maudhui yamigogoro ya kijamii uhakiki chozi la kheri

0 comments

 

 

  KWA KUREJELEA RIWAYA YA CHOZI LA HERI, FAFANUA MAUDHUI YA MIGOGORO YA KIJAMII.

Mgogoro ni hali ukinzani fulani ambao mhusika anaweza kukumbana nao hasa anapoyajenga maudhui ya kazi ya fasihi. Mhusika anaweza kuwa na mgogoro wa kindani ambao husababishwa na yeye mwenyewe kifikra hasa anapojaribu kuyatatua maswala fulani kuhusu mazingira yake. Kwa upande mwingine ipo migogoro inayosababishwa  na mwingiliano kati ya mhusika na wahusika wengine katika kazi ya fasihi.

Kumekuwa na ongezeko la migogoro   katika jamii mbalimbali. Kumekuwa na ugomvi, vita, talaka na hata mauaji katika jamii mbalimbali. Migogoro katika jamii zetu husababishwa na misimamo tofauti ima ya mtu binafsi au jamii fulani kwa jumla. Kwa hivyo migogoro ni mivutano na mikinzano mbalimbali katika kazi ya fasihi.

Wakati mwingine migogoro inaweza kuwa na mizizi yake katika familia zilizomo katika kazi teule ya fasihi. Kila familia huwa na misimamo na mbinu ya kipekee ya kukabiliana na maisha . Utofauti huu ambao Waaidha uneweza kuwa unasukumizwa na mielekeo ya kibinafsi kifamilia huleta dhana ya mgogoro huku ikizingatiwa kuwa kila jamii inaandama maisha kivyake.

Mbali na hayo migogoro inaweza kutokea kwenye misingi ya kitabaka. Katika msingi huu tabaka la juu hujiona kuwa bora kuliko lile la chini huku likilikandamiza tabaka la chini. Kwa upande wake lile la chini hujiliwaza kwa imani kuwa kila kiumbe ni bora machoni pa Muumba. Hali ya ukinzani hudhihirika wazi hasa matabaka haya mawili yanapojikuta katika  shughuli fulani ya kijamii. Hata hivyo tabaka la juu huongozwa na kiburi na dharau dhidi ya hali duni ya tabaka la chini.

Nyadhifa mbalimbali za kikazi au madaraka, wakati mwingine huzua hali ya mgogoro kati ya watawala na watawaliwa. Wakati mwingine watawala huwakandamiza watawaliwa kwa kuwanyanyasa na kuwasahaulia mbali kwa kutaka maamuzi yao pekee ndiyo bora. Hali hii inapotokea basi ukinzani hujitokeza moja kwa moja kati ya makundi haya mawili.

Migogoro vile vile inaweza kusababishwa na hali tofauti ya kiuchumi katika jamii zilizomo kwenye kazi ya fasihi. Pia nafasi tofauti ambazo wahusika wanazo huwa pia hoja changizi katika makuzi ya migogoro bila kusahau hali tofauti za misimamo ya wahusika kisiasa.

 

Katika riwaya ya Chozi la Heri migogoro imejitokeza katika wahusika na viwango mbalimbali.Migogoro hii imewaathiri wahusika binafsi pamoja na jamii nzima ya uhusika katika kazi hii. Migogoro hii imejadiliwa kwa mapana kama ifuatavyo:-

Kuna mgogoro kwenye familia ya Mzee Mwimo Msubili, kwa sababu familia yake ilikuwa kubwa na hakuitosheleza kwa chakula. Uk 9,"Wingi wa vinywa vya kulishwa ulizua uhasama, migogoro na hata uhitaji mkubwa "

Mgogoro huu uliiandama familia ya Mzee Mwimo Msubili vikali sana. Kwanzia ukurasa wa tisa tunaona vile jamii yake inavyoana kubanana katika vipande vidogo vidogo vya ardhi kwa kuwa ni wengi kuliko ardhi aliyoimiliki Mzee Mwimo Msubili. Mwandishi anaichora taswira hii kwa kurejelea hali halisi ya kimaumbile ambapo kitu chcochote kinapobinywa na kukandamizwa hujaribu kufurukuta ili kupata nafasi ya kupumua.

Mgogoro huu ulimsababisha Mzee Mwimo kuwatafutia wanawe Hifadhi wajinusuru na hali hiyo ngumu katika kuwahamishia wake wawili wa mwisho kwenye Msitu wa Heri au Ughaishu kama walivyouita watu wa huko. Hii ndiyo iliyokuwa njia ya pekee ilisalia ili kutatua hali iiyomkabili Mzee Mwimo Msubili. Huko alikowahamishia kulikuwa afueni kwani waliweza kupata vipande vya ardhi na kuvitumia vilivyo ili kukidhi haja zao za kucha kutwa zikiwa ni pamoja na kupata maakuli ya kuitosheleza jamii hii.

Upo mgogoro mwingine  wa kijamii unajitokeza baada ya mkoloni kupuuza sera za Mwafrika.Uk 10,"Hatua ya mkoloni ya kupuuza sera za Mwafrika za umiliki wa ardhi na kuamua kujumuisha pamoja ardhi iliyomilikiwa na mtu binafsi na kuuidhinisha umiliki huu kwa hatimiliki, ilivuruga mshikamano wa kijamii "Kwa yakini wakati wa uvamizi wa mataifa yanayoendelea na mkoloni, hali ambayo haikusazwa ni ile ya kuyanyakua mashamba ya wakazi asilia huku wakoloni wakijilimbikizia mashamba pasi kujali athari hizo kwa wenyeji. Mkoloni alifanya hivi kwa kupuuza sera za Mwafrika za kumiliki ardhi na kuamua kujumuisha pamoja ardhi iliyomilikiwa na mtu binafsi, na kuidhinisha kijamii. Katika sera ya kijadi ya umiliki na matumizi ya ardhi, raia wote, hata wageni, walikaribishwa na kugawiwa mashamba, hivyo kupata mbinu za kujiendeleza kimaisha.

Mgogoro ulizua utata baina ya jamii asilia na zile za wakoloni kwani uhasama uliokithiri na kukolea akilini mwa waja. Wale walioyamiliki mashamba kabla ya kuja kwa wakoloni, waliohisi kuwa ukoloni umewavamia na kuteka nyaya rasilmali yao ya ardhi. Hali hii ilisababisha chuki baina ya waathiri na waathiriwa kwa kuwa urasmi wa umiliki wa ardhi yao uliwatoweka na kunaswa na wakoloni ambao licha ya kuwanyanganya ardhi yao waliwafanya watumwa.

Kwa upande wa wenyeji, kulizuka hali ya uhasama kwa kuona kuwa wale Waliokosa mahali pa kujisitiri wakajiona kama wasiofaa katu. Wengine hasa waliopoteza mashamba yao na kulazimishwa kuyafanya ya kitaifa. Mgogoro huu ulisababisha uhasama ambao kuondoa si rahisi na pia mgogoro kama huu, huhamisha na kuathiri ujumla wa waathiriwa na jamii kwa jumla katika nyanja mbalimbali.

Kulijitokeza mgogoro shuleni wakati Ridhaa aliitwa 'mfuata mvua',na kutengwa na wenzake. Uk 10,"Wewe ni mfuata mvua. Hatutaki kucheza nawe. Umekuja hapa kutushinda katika mitihani yote. Wewe ndiwe unayetuibia kalamu zetu "Walimwona kama mwizi. Ridhaa alikuwa mojawapo wa waathiriwa na ubaguzi akiwa shuleni.Aliweza kutengwa na wenzake hasa walipokuwa wakichaeza mchezo wao wa Kavuta ambao unachezwa na kupendwa sana na watoto wa kusukuma Vifuniko vya chupa za soda kwa ncha za vidole vyao. Hali hii ilimwathiri sana Ridhaa na hata alipofika nyumbani kwao akajitupa sakafuni na kulia kwa kite na shake. Mama yake alipowasili hakusita ila kupendekeza asirudi shuleni kwa kuhofia kuchekwa na wenzake kila mara.

Hata hivyo mama mtu anampa wosia kuwa asiwe mtu wa kutoka tamaa kwa haraka hasa akiwa shuleni.Shule ama elimu  aione kama chombo cha kueneza amani na upendo wala sio fujo na chuki. Alizidi kumshauri kuwa huenda mwenzake alikuwa na hofu kwa vile alionao uhuru wake umeingiliwa. Na kutokana na ushauri huo, Ridhaa akapata mwanzo wa maisha ya heri.uk.11.

Ridha kibinafsi anajikuta katika mgogoro katika nafsi yake mwenyewe. Uk 12,"Miguu yake sasa ilianza kulalamika pole pole parafujo za mwili wake zililegea, akaketi juu ya ya wapenzi wake. Baada ya muda wa mvutano, wa hisla na mawazo, usingizi ulimwiba. Hii ilitokana na kugundua kuwa mahali alipoishi hapakuwa pake haswa tangia mwanzoni. Hii ilitokana na dalili za vitushi ambavyo vilimwandama. Anajaribu kupiga taswira nyuma kuhusu namna alivyokuja kumiliki kipande cha ardhi alichokijengea nyumba yake kwa kuuziwa na dadake Kendi sehemu hiyo ikiwa msitu.

Alitia juhudi kuhakikisha kijiji kizima kinapata maji safi ya mabomba ambayp maji haya yaliweza kubadili mazingira ya pale yaliyokuwa sawa na jangwa la Kalahari hadi kuwa ardhi ya chanikiwiti yenye rutuba si haba. Maswali chungu nzima yalimwandama akilini akakose majibu.

Hakujua apige ukemi au afanyeje. Akiwa katika hali hiyo ya mgogoro wa kinafsia, ndipo anaanza kukumbuka na kuelewa  mambo mbalimbali yaliyokuwa yakitendeka kama kusambazwa kwa vikaratasi vikiwatahadharisha kuwa kulikuwepo na gharika mbeleni baada ya kutawazwa kwa Musumbi(Kiongozi) mpya, kukatwa kwake mguu na jirani yake mara moja pamoja na ile hali ya mke wa jirani yake kulalamikia kuuzwa kwa shamba la wenyeji kwa wageni.

Kulikuwa na mgogoro uliosababishwa na wanasiasa, juu y nani atakaye kuwa kiongozi wa jamii, kati ya mwanamke mwananume. Uk 19,"MijadaIa hii ilizua na kukuza migogoro isiyomithilika ". Kuhusu hali hiyo mgogoro huu uliathiri hali mbalimbali za eneo hilo. Kila kikundi kilikuwa kikiunga mkono msimamo wao.

Matokeo yake yalikuwa pamoja na kutenda kwa hali ya taharuki ilitanda ambapo vyombo vya madola vikatumwa kudumisha Usalama katika vijiji, mitaa nayo ikajaa polisi wa kuzima vurugu katika kila pembe. Kuwepo kwa vikosi vya polisi katika mitaa ya watu hakukusaidia chochote bali kulizidisha migogoro baina ya pande hizo mbili hasimu. Kila upande uliona kuwa huenda ikawa walienda Usalama walikuwa na nia ya kuwaondoa viongozi waliowapigia debe madarakani.

Baada ya kura wagombezi wote walijikalia majumbani mwao  na kuwatazama kwenye runinga namna Wafuasi wao walivyozozana. Katika hali hii mchezo wa pata shika polisi kukimbizana na raia huwa jambo la kawaida. Ikumbukwe kuwa raia huwa hawana silaha hatari kama walizo nazo polisi hivyo basi hii hupelekea kuuawa kwa watu wasio na hatia kiholela huku polisi wakinadi kuwa wanatuliza vurugu.

Mgogoro mwingine ulijitokeza kati ya raia na wanapolisi, wakiwa katika harakati zao za kuweka amani. Uk 19,"Mchezo wa polisi kukimbizana na raia ulianza katika mchezo huo mamia ya roho zisizo na hatia zilisalimu amri chini ya pambaja za risasi na mapigo ya rungu, vitoa machozi navyo vikafanya kazi barabara. Hii ilitokana na hali ya kuweka usalama baina ya wafuasi wa wagombezi hao. Hii husababisha polisi kujipata kwenye mgogoro mkubwa na raia wasio na hatia.

Walinda usalama huajaribu kwa jino na ukucha kutumia mbinu zozote zile mradi zitawasaidia kukomesha vurugu baina ya Wafuasi ingawa Wafuasi hawa nao huwaona polisi kama adui wao mkubwa ambaye ana nia ya kuwazuia kutekeleza katiba yao kama demokrasia ya nchi inavyonadi.

g)Nyamvula anajikuta katika mgogoro wa nafsi yake, wakati ambapo imani yake inakinzana na kazi ya kuwa askari. Uk 62,"Kulingana na Nyamvula, kuwa askari wa vita kulikinzana na imani yake, hasa kwa vile Nyamvula alisema ni born again. Mwangeka alimsisitizia kuwa kulinda usalama si sawa na kuua " Hapa Nyamvula anajikuta katika njia panda asijue la kufanya hasa baada ya rafiki yake kumithilisha kazi ya ulingaji usalama na dhambi ikichukuliwa kuwa Nyamvula ni mwokovu. 

Katika ukurasa wa 38 Tila anaitaja migogoro kadha iljYO katika Tamthilia ya Hussein. Tamthilia hii ya Mashetani ninayorejelewa ina migogoro mingi sana kama: migogoro ya kisiasa, kiuchumi, na pia ya kijamii.

"Tila:

Nadhani umesahau baba. Suala hili ulisema limeshUghulikiwa katika kazi za kifasihi kama vile Mashetani, ile tarnthilia ya Hussein inayoisawiri migogoro ya kisiasa, kiuchumi na kijamii ya baada ya ukoloni lsitoshe, mwalimu alitaka tu kuonyesha  kwamba upo uhusiano kati ya mfumo wa kiuchumi na mfumo wa kisiasa alituambia kwamba mfumo wa kiuchumi hudhibitiana na mfumo wa kisiasa. Utawala huteuliwa makusudi kuendeleza mfumo uliopo wa kiuchumi kwa maslahi ya watawala na tabaka ambalo linazimiliki nyenzo za uzalishaji mali "

Mbali na aina hii ya migogoro, pia kuna ile migogoro inayoletwa na tofauti katika hadhi za maisha ambapo kuna walaheri na walalahoi. Katika kazi hii ulalahoi unadhihirika katika wahusika kadhaa. Tunapata kuwa waafrika wanajikuta katika hali ya umasikini; Uk 7,"Waafrika waliobahatika kuwa na makao yao binafsi walipata sehemu ambazo hazingeweza kutoa mazao yenyewe; na bila shaka hali yao iliweza kutabirika; kuvyazwa kwa tabaka la wakulima wdogowadogo, maskini, wasio na ardhi "

Uk 25,"Nyinyi ndio vikaragosi wanaotumiwa na wasaliti wa nia zetu kuendelea kutudidimiza kwenye lindi hili la ukata "

Ridhaa pia anajikuta kwenye lindi la umaskini baada ya mali yake yote kuchomwa, ikiwemo familia yake.

Uk 1,"Ridhaa alisimama kwa maumivu makali, mikono kairudisha nyuma ya mgongo wake uliopinda kwa uchungu. Macho yake yaliyotanda ukungu  alikuwa kayatunga juu angani, akitazama wingu la moshi lililojikokota kwa Kedi na mbwembwe; wingu lililomwonyesha na kumkumbusha ukiwa aliozaliwa nao na ambao alihofia kuwa angeishi na kuzikwa nao. "

Tunapata pia kuwa watu wengi wanaiaga dunia wakijaribu kujikomboa kutokana na hali hii ya ukata, wanapoenda kuchota mafuta kwenye lori ambalo limebingirika kisa na maana alienda kuwaokoa watu ambao wa likuwa wakipora mafuta kutoka kwenye lori, ambalo lilikuwa limebingiria lnasemekana kuwa umaskini uliwasukuma watu hawa kuchukua kisichokuwa haki yao!"

Hii ni kuwa hali hizi mbili tofauti zina ukinzani mkubwa ambao huzua migogogro kati ya wahuka wanaopatikana katika kila pende.

Swala la ushirikina pia limezua mgogoro wa imani kati ya jamii na kuchukuliwa kuwa mojawapo wa nguzo zao za kimaisha. Hata hivyo, wasio na imani kama hiyo hujikuta katika mrengo pinzani ambao huleta mgogoro katika jamii husika.

Ridhaa anaposikia milio ya bundi, anaamini kuwa milio hii ina maana iliyofichika. Uk 1,"Anakumbuka mlio wa kereng'ende na bundi usiku wa kuamkia siku hii ya kiyama. Milio hii ndiyo iliyomtia kiwewe zaidi kwani bundi hawakuwa wageni wa kikaida katika janibu hizi " Uk 2,"Ninashangaa ni vipi daktari mzima hapo ulipo unajishughulisha na mambo ya ushirikina.

Swala la migogoro pia halikusaza familia mbalimbali katika kazi hii.Mwangeka alikutana na Lily Nyamvula katika Chuo kikuu na kumwoa. Walibarikiwa na mtoto mmoja kwa jina Becky.

Ndoa hii haikudumu kwani Lily na Becky waliangamia kwenye janga la moto.Baada ya ndoa ya mwanzo kusambaratika, Mwangeka alimwoa Apondi. Walibarikiwa na mwana wa kiume kwa jina Ridhaa.

Mwangemi alimwoa mwanamke kwa jina Neema. Hawakufaulu kupata mwana wao kindakindaki japo walipanga mwana wao kwa jina Mwaliko. Hii ilisababisha migogoro katika jamii hii kwa kukosa kufahamu chanzo chao cha kutofanikiwa kupata mtoto.

Lucia Kiriri —Kangata-,-alikuwa ameolewa katika ukoo wa Waombwe ambao awali walikuwa maadui sugu wa ukoo wa Anyamvua. Ndoa hii ilipata pingamizi sana kutoka kwa ukoo mzima lakini kutokana na Msimamo imara wa Kangata ndoa hii ilisimama. Watu wa ukoo wa kina Kangata walishangaa ni kwa nini mwana wao akaozwa kwa watu ambao huvaa nguo ndani nje na pia huzaa majoka ya mdimu ambayo ni machoyo kupindukia.

 

Lunga alikuwa na mke kwa jina Naomi. Walikuwa na wana watatu, Umu, Dick na Mwaliko. Ndoa hii haikudumu kwaniNaomi alimwacha Lunga na kwenda mjini alikokuwa shangingi kwelikweli. Hii ilikuwa kwa sababu za migogoro ya mara kwa mara nasfi ya Naomi ya kutaka uhuru wa kushiriki anasa atakavyo pamoja na kukataa kutii kama mke katika ndoa yake.

Pete na Fungo- tunaelezwa kuwa Pete alipoingia darasa Ia saba alipashwa tohara nao wajombake wakapokea posa na baadaye mahari kutoka kwa buda mmoja kwa jina Fungo aliyemuoa kama bibi wa nne. Ndoa hii haikudumu kutokana na kutoaminiana kati ya  wanandoa hawa na mwishowetunajuzwa kuwa  kwani Pete alihiari kumwacha baba huyu kwa kuwa alionao si makamo yake katu.

Suala la ukoloni nalo pia limechangia pakubwa kuwepo kwa migogoro katika kazi hii. Ukoloni  mamboleo ni zao la uongozi mbaya. Viongozi waanzilishi wa mataifa yaliyopata uhuru hawakuzua sera na mikakati mwafaka ya kuhakikisha nchi zao zimepata kujisimamia kiuchumi.Misimamo hii inaleta mafarakano katika jamii husika kama inavyojitokeza katika kazi hii.

Katika Chozi la Heri, Waafrika wenyewe wanajifanya wakoloni juu ya waafrika wenzao, ambao wako chini yao kitabaka au kisiasa kwa mfano katika ukurasa wa 5,mashamba ya Waafrika yananyakuliwa na watu binafsi baada ya wakoloni kwenda, nao waafrika wanawekwa mahali pamoja ili kuishi katika hali ya ujamaa "Lakini baba, wewe siwe uliyeniambia kuwa mashamba ya Theluji nyeusi yalikuwa milki ya wakoloni?na sasa yanamilikiwa na nani? Si mwana wa yule mlowezi maarufu ambaye wewe hunitajia kila mara? Maekari kwa maekari ya mashamba katika eneo Ia kisiwa bora yanamilikiwa na nani? Si yule myunani aliyewageuza wenyeji kuwa maskwota katika vitovu vya usuli wao?"

Katika ukurasa wa 24 tunapata kuwa vijana wanakufa kwa mitutu ya bunduki wanapojaribu kujikomboa kutokana na ukoloni wa Mwafrika. Walipigania uhuru wa tatu, ambao ni ukombozi kutokana na uongozi wa Mwafrika "Baada ya muda mfupi, vifua vyao vilikabiliana na risasi zilizorashiwa vifua hivyo kama marashi, vifua vikawa havina uwezo dhidi ya Shaba, vijana wakaanguka mmoja baada ya mwingine, wamekufa kifo cha kishujaa, wamejitolea mhanga kupigania uhuru wa tatu"

 

Vile vile ukoloni mkongwe nao pia una mchango mkubwa katika kuwepo kwa migogogro katika kazi hii.Huu ni ukoloni uliokuwa wa Waingereza, kabla ya nchi za  Afrika kupata uhuru.

Tunapata kuwa mkoloni anapata fursa ya kuendeleza kilimo katika sehemu za mashamba ya Waafrika zilizotoa mazao mengi. Uk 7, "Mustakabali wa ukuaji wetu kiuchumi uligonga mwamba wakati sheria ya mkoloni ilipompa mzungu kibali cha kumiliki mashamba katika sehemu zilizotoa mazao mengi. Ukengeushi wa ardhi ukatiliwa muhuri, umilikajia wa ardhi na Mwafrika katika sehemu hizi ukapigwa marufuku; si mashamba ya chai, si ya kahawa yote yakapata wenyeji wageni dau la mwafrika likagonga jabali.Hali kama hii inazua migogoro katika ya wakoloni na wenyeji asilia wa eneo linaliathirika.

Katika ukurasa wa 7 tunasoma; "Waafrika waliobahatika kuwa na makao yao binafsi walipata sehemu ambazo hazingeweza kutoa mazao yenyewe; na bila shaka hali yao iliweza kutabirika; kuvyazwa kwa tabaka la wakulima wadogowadogo, maskini, wasio na ardhi. Nadhani unaweza kukisia hali ilivyokuwa kwa familia nyingi za kiafrika. Kama vile baba

Msumbili alivyokuwa akisema, jamii yetu iligeuka kuwa hazina kuu ya wafanyakazi ambamo wazungu wangeamUa kuchukua vubarua kupalilia mazao yao"

Tunaona kuwa wazungu bado waliwatumia waafrika kama wafanyakazi mashambani 'mwao',ambayo walinyakL kutoka kwa waafrika.

Ipo vile vile migogoro inayozaliwa kwenye misingi ya kifeministi ambapo mwanamke anakosa kutambulika kama kiembe kilicho imara na chenye usemi katika jamii. Pasi jinsia zote mbili kutambulika migogoro katika jamii husika hudumu mile daima.

Katika ukurasa wa 16 tunasoma; "Siku ile baada ya kutawazwa kwa kiongozi mpya, kiongozi ambaye kulingana na desturi za humu mwetu, hakustahili kuiongoza jamii ya wahafidhi na, kisa na maana, alikuwa mwanamke.

Katika ukurasa wa 3;"Huku ni kujiumbua hasa. Unyonge haukuumbiwa majimbi; ulitunukiwa makoo.Bibi alikuwa akimwelezea Ridhaa kuwa unyonge haukuumbiwa 'majjmbi'ambao ni wanaume, bali uliumbiwa 'makoo',yaani wanawake. Hivyo basi tunapata kuona kuwa jamii pia iliwadhalilisha wanawake tangu zamani.

Katika ukurasa wa 8; "Mzee mwenye wake na wana wengi alihesabiwa kuwa mkwasi kwelikweli basi wake hawa hawakuchelea kutimiza amri ya

maumbile, wakapania kuujaza ulimwengu " Tunapata kuwa wanawake wanadhalilishwa kwa kuonekana kana kwamba jukumu lao kuu katka jamii ni kuijaza dunia au kuzaa wana. Mwanamke hapewi nyadhifa za umuhimu katika jamii ila tu kazi yake ni kuoleka na kujaaliwa na wana wengi awezavyo.

Katika ukurasa wa 45;"Viongozi wengi wa awali walibwagwa chini na vijana chipukizi. La kuhuzunisha ni kwamba wengi walishindwa kabisa kukubali ushinde, hasa yule ambaye alikuwa anagombea kilele cha uongozi. Kulingana naye, nafasi hii iliumbiwa mwanamume, na kupewa mwanamke ni maonevu yasiyovumilika "Katika hali hii, jamii haikukubali wanawake kuwa viongozi, bali cheo hiki cha uongozi kilikuwa cha jinsia ya uwsanaume.

 

Katika ukurasa wa 149; "Maisha yangu na Fugo yalikuwa kama ya ng' ombe aliyetiwa shemere na kufungwa nira pamoja na punda ambaye anakaidi kusonga. UIe unene wake, lile kituzi lililotoka kwenye makwapa yake makuza na kUfudikiza kote chumbani, ule wivu wa mke mwenzangu wa

pili, kule kukemewa na kuchekwa na watoto wa mke wa kwanza yote yalininyong' onyeza na kuniumbua. Nilichukia jaala aliyonipa mama kwa kujali maslahi yake tu, nilichukia nguvu ya maumbile iliyoniweka kwenye jinsia ya kike, nilichukia kitoto nilichohimili kwenye mji wangu hata miezi tisa ilipotimia na kupata salama, niliamua kwamba kwa mzee Fungo hakuniweki tena.

Na unadhani anakwenda wapi?Utawezaje kujitunza wewe na mtoto wako na hali bibi yako ndiye huyohana hanani, na wazazi wako walafi walikuuza kwangu ili wapate pesa za kuwasomesha ndugu wako watano wa kiume?AliulizaFungo "Tukio hili linatuonyesha wazi jinsi mwanamke amedhalilishwa katika jamii. Hivyo basi jamii haikosi kuwa na migogoro hadi hapo mwanamke atakapopewa nafasi yake.

Kwanza, mamake mtoto huyu msichana anamwoza kwa mzee mwenye wake wawili, (Mzee Fungo),ili aweze kupata pesa za kuwalipia vijana wake karo ya shule.

Msichana anaonekana kutokuwa na umuhimu ya kupelekwa shuleni ili kupata elimu, ilhali yeye mwenyewe aliazimia kuendeleza masomo yake. Maazimio yake ya elimu yanagonga mwamba baada ya kuozwa ka mzee Fungo ambaye anamtesa na mwishowe kumtaliki na kitoto kichanga.

Msicha na huyu mchanga pia anapitia machungu kwenye ndoa yake kwa kuchekwa na kudharauliwa na wake wenzake na wana wao.

Hitimisho.

Migogoro huweza kuwa kati ya wahusika ambapo wahusika hawa huwa na misimamo inayotofautiana kabisa kuhusu hali tofauti za kimaisha. Mgogoro kama huu huonekana kana kwamba umeipiku migororo mingine yoyote ile kwa kuwa matukio yote katika kazi yoyote ya fasihi huendeshwa na kuelekezwa kupitia viumbe hawa. kwa kuwa suala la migogoro limekuwa tatizo sugu katika jamii zetu, ipo haja ya kujaribu kwa vyovyote  kuona kuwa jambo hili linapata tiba ya kudumu.

Marejeleo.

a.     Bouchier D. The Feminist Challenge. London: Macmillan Press, 1983.

b.     Burleson B, Denten W. The Relationship between Communication Skills and Marital Satisfaction: Some Moderating Effects. Journal of Marriage and Family,1997; 59(4).

c.      Chapman G. Desperate Marriage. Moving towards Hope and Healing in Your Relationship. Chicago: Northfield Publishing, 2008.

d.     Mugenda O, Mugenda A. Research Methods: Quantitative and Qualitative Approaches. Nairobi: Acts Press, 1999.Ogechi N. Mbinu za Mawasiliano. Eldoret: MoiUniversity Press, 2002.

e.      Wamitila K. Uhakiki wa Fasihi, Misingi na Vipengele Vyake. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd, 2002.

f.       Republic of Kenya The Constitution of Kenya, 2010: Kenya Gazette Supplement. Nairobi: The Government Printers, 2010.

g.     Assumpta, K.H(2014). Chozi la Heri, One planet Publishing & Media services Limited, Nairobi.

h.      TUKI, (2004) Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Oxford University Press: Nairobi.

i.       TUKI  (1990) Kamusi Sanifu ya Isimu na Lugha .   Dar es Salaam, University of Dares Salaam.

j.       Wafula, R.M.& Kimani Njogu (2007).  Nadharia za Uhakiki wa Fasihi.  Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

k.     Wafula, R.M. (1999).  Uhakiki wa Tamthilia: Historia na Maendeleo Yake.  Nairobi:  Jomo Kenyatta Foundation.

l.       Wamitila, K.W. (2003).  Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia.  Nairobi: Focus Books.

m.  Wamitila, K.W.  (2002).  Uhakiki wa Fasihi.  Nairobi: Phoenix.

 

 

 

  

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment