FAFANUA MCHANGO WA
FASIHI ILIYOTAFSIRIWA JUU YA FASIHI SIMULIZI....
Utangulizi
Kwa muda sasa, kumekuwepo na ongezeko kubwa
la kazi za Kiswahili zilizotafsiriwa kutoka katika lugha zingine mbalimbali.
Ongezeko hili limechangia pakubwa katika kuwepo kwa kazi nyingi za fasihi ya
Kiswahili ikiwemo fasihi simulizi. Tamthilia, riwaya, hadithi fupi, mashairi,
pamoja na tanzu mbalimbali za fasihi simulizi na hata tungo zingine katika
lugha za kigeni na za kiafrika sasa zinaweza kusomwa katika lugha ya Kiswahili.
Mchango huu mkubwa bado haujatambuliwa na wasomi wengi ambao miongoni mwao ni
wale wanaofaidika na tafsiri hizi.
Tafsiri hizi hata hivyo zimeandamwa na
changamoto chungu nzima katika kuhakikisha kuwa tunapata tafsiri faafu za kazi
za lugha ya kigeni. Hivyo basi, kazi hii inalenga kudadisi mchango wa kazi
zilizotafsiriwa katika kuendeleza lugha na fasihi ya Kiswahili pamoja na
kuchanganua changamoto zinazoambatana na tafsiri za kazi hizi. Aidha, makala
haya yanalenga kuonyesha umuhimu wa kudhamini kazi hizi, kuzichunguza upya tena
kwa nia ya kuzikosoa na zaidi ya yote kupendekeza njia mwafaka za kuibuka na
tafsiri faafu katika karne hii ya teknolojia na utandawazi.
Maana ya
tafsiri
Kulingana na
Larson (1994), tafsiri ni neno linalotumiwa kumaanisha harakati ambapo maana ya
maelezo katika lugha moja ambayo ni lugha chasili inabadilishwa hadi maana ya
lugha nyingine ambayo ni lugha lengwa. Pia, Newmark (1988), anasema kuwa
kutafsiri ni kitendo cha kubadilisha kauli au habari iliyoandikwa kwa lugha moja
hadi lugha nyingine.
Tafsiri
hufanywa kwa lengo la kutaka ujumbe fulani ulio katika lugha isiyoeleweka
kueleweka na wasomi. Crystal (1987), anasisitiza kauli hii kwa kusema kuwa watu
wanapokabiliwa na lugha wasiyoielewa, humwendea mtafsiri ili waweze kufasiri
habari hizo. Hii ni kumaanisha kuwa kitendo cha kutafsiri hutatua shida za
kutoeleweka kwa ujumbe katika lugha iwayo yoyote. Mtafsiri huhitajika kuonyesha
ulinganifu, mshikamano na pia usambamba kati ya lugha zote mbili anapofanya
tafsiri.
Tafsiri ni taaluma
ambayo imeshughulikiwa kwa muda mrefu na wataalamu mbalimbali. Mbali na fasihi,
taaluma hii imehusisha nyanja zingine za kitaaluma kama vile isimu, filosofia,
na hata mawasiliano, (Munday (2001).
Kwa upande wa
tafsiri, Catford akinukuliwa na Mwansoko (2006) anasema tafsiri ni kuchukua
mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha moja (lugha chanzi) na kuweka
badala yake mawazo yanayolingana katika lugha nyingine (lugha lengwa).
Naye Newmark
(1982) anaeleza kuwa tafsiri ni mchakato wa uhawilishaji wa maneno kutoka
matini chanzi kwenda matini lengwa.
Pia Nida na
Taber (1969) wanaeleza kuwa tafsiri hujumuisha kuzalisha upya ujumbe wa lugha
chanzi kwa kutumia visawe vya asili vya lugha lengwa vinavyo karibiana zaidi na
lugha chanzi kimaana na kimtindo. Wao wanatilia mkazo uzalishaji upya wa kwa
kutumia visawe asili vinavyokaribiana na matini chanzi kimaana na kimtindo.
Kutokana na maana hizi tunaweza kusema kuwa tafsiri hufanywa katika ujumbe
uliopo katika maandishi, ni jaribio la kiuhawilishaji na wazo linalatafsiriwa
huwa na visawe vinavyokaribiana na sio sawa kutokana na tofauti za kiisimu,
kihistoria, kiutamaduni na mazingira.
Kwa ujumla
tafsiri ni mchakato wa uhawilishaji wa mawazo, ujumbe au maana katika maandishi
kutoka lugha moja hadi nyingine (kutoka lugha chanzi kwenda lugha lengwa).
Kwa hivyo,
tafsiri ni taaluma ya uhawilishaji wa mawazo katika maandishi kutoka lugha
chanzi kwenda lugha lengwa kwa kuzingatia isimu, mukutadha na utamaduni.
Taaluma ya tafsiri imeanza hivi karibuni mara baada ya majilio ya maandishi.
Hii ina maana kwamba baada ya kuwepo kwa maandishi ndipo taaluma hii ya tafsiri
ikaanza.
Taaluma hii ya
tafsiri huhusisha stadi kuu nne za muhimu ambazo ni kusoma, kuandika,
kusikiliza na kuzungumza. Mfasiri anatakiwa kuwa na ujuzi wa taaluma hii ili
kufanikisha mchakato wa tafsiri kwa ufanisi.
Mchango wa
kazi zilizotafsiriwa katika uga wa fasihi andishi na simulizi.
Taaluma hii
imeendelea kukua kadiri muda unavyosonga. Kwanza kabisa, tafsiri imechangia
kuwepo kwa ongezeko kubwa la kazi za Kiswahili zilizotafsiriwa kutoka katika
lugha zingine.. Ongezeko hili limechangia kuwepo kwa kazi nyingi za fasihi ya
Kiswahili. Tamthilia, riwaya, hadithi fupi, mashairi na hata tungo zingine
katika lugha za kigeni na za kiafrika sasa zinaweza kusomwa katika lugha ya
Kiswahili. Yaani imeweza kuitajirisha fasihi ya Kiswahili. Vitabu vingi vya
lugha ya kigeni hasa ya Kingereza vimetafsiriwa kwa Kiswahili na hivyo
kupigisha hatua fasihi ya Kiswahili. Baadhi ya kazi hizi ni kama vile: The Well
of Giningi - Kisima cha Giningi, Maisha Yangu “Moya Zhizn”, riwaya ya Andrei
Zhukov 1968 Kiswahili-Kirusi, I will marry when I want - Nitaolewa Nikipenda,
The Beautiful Ones are Not yet Born - Wema Hawajazaliwa, The Taste of Heaven -
Aliyeonja Pepo Tamthilia, The Government Inspector - Mkaguzi Mkuu wa Serikali
Tamthilia Christon Mwakasaka 1979 Kiingereza-Kiswahili, Anthology of Swahili
Poetry - Kusanyiko la Mashairi, The Black Hermit - Mtawa Mweusi , Song of
Lawino - Wimbo wa Lawino miongoni mwa kazi nyingi maarufu.
Kazi hizi
ambazo zimetafsiriwa katika mfumo wa fasihi andishi ndizo zizo hizo ambazo
zinatimiza mahitaji ya fasihi simulizi kwani hali ni ile ile isipokuwa njia ya
uwasilishaji.
Ifahamike kuwa
kazi hizi sasa zinasomeka kwa Kiswahili. Ni malighafi ya fasihi ya Kiswahili
kutokana na mchango wa tafsiri.
Kutokana na
tathmini ya kina, imedhihirika kuwa tafsiri hizi za kazi ya fasihi zimefanywa
sana katika kitengo cha tamthilia kuliko riwaya, hadithi fupi na Mashairi.
Mwansoko (2006:46) anaeleza kuwa tamthilia ni utanzu uliotafsiriwa sana
kutokana na malengo makuu mawili; lengo la kuigizwa na lengo la kusomwa. Pia
umefasiriwa sana kutokana na kwamba, ulikuwa ni utanzu mpya katika Afrika,
hivyo wageni na wenyeji walitafsiri kwa lengo la kuutambulisha katika mazingira
ya kiafrika. Vilevile umeonekana kutafsiriwa sana kutokana na urahisi wa lugha
yake, kwani tamthilia hutumia maneno machache na yanayoeleweka tena bila hata
ya ufafanuzi wa kina kama ilivyo katika riwaya. Zaidi ya yote, umefasiriwa sana
kutokana na umuhimu wa maudhui yake ambayo hujibainisha katika masuala mtambuko
duniani kote. Kwa mfano; tamthilia ya “Nitaolewa Nikipenda na Mtawa Mweusi”
maudhui yake yanahalisika katika jamii mbalimbali. Vilevile umetafsiriwa sana
kwa lengo la kukuza na kueneza lugha adhimu ya Kiswahili, ambayo haikuwa na
machapisho mengi yahusuyo fasihi andishi. Kwa upande wa lugha zilizojitokeza
zaidi katika kufanikisha suala la tafsiri ya fasihi ya Kiswahili ni lugha ya
kiingereza, na Kiswahili; lugha ya Kiingeza imejitokeza sana katika tafsiri
kutokana na kwamba, waingereza ni moja kati ya mataifa yaliyotawala sehemu
kubwa ya dunia, na ndio taifa lililokuwa na dola yenye nguvu zaidi. Vilevile Waingereza
walishapiga hatua kubwa katika maendeleo ya fasihi ima andishi au simulizi ukilinganisha
na mataifa mengine. Pia hata lugha ya Kiingereza ni moja kati ya lugha kubwa
duniani na inayofahamika na mataifa mengi. Lugha ya Kiswahili nayo imeonekana
kutafsiriwa sana kutokana na hitaji la kuwa na machapisho mengi ya kifasihi ili
kukuza na kueneza fasihi ya Kiswahili. Pia ni lugha inayokua kwa kasi na
inayoeleweka sana Afrika Mashariki ukilinganisha na lugha nyingine.
Pili,
imewezesha ulinganisho wa utamaduni wa Kiswahili na ule wa kigeni. Tafsri
hutusaidia kujua na kulinganisha tamaduni za jamii nyingine na ile
iliyoandikiwa tafsiri. Tamthilia ya “Nitaolewa Nikipenda” imetungwa katika
mazingira ya jamii ya kikuyu, hivyo tafsiri ya tamthilia hii imesaidia kujua
utamaduni wa Wakikuyu. Kwa mfano katika ukurasa wa 65, tunaweza kuona jinsi
ndoa ya kikuyu inavyofungwa, utaratibu wa utoaji mahari pamoja na nyimbo
ziimbwazo wakatika wa sherehe. Ni muhimu kutaja kuwa kipengele cha utamaduni
huwaathiri pakubwa tafsiri. Kulingana na Teilanyo (2007:16) utamaduni ni chanzo
cha utata katika kutafsiri anaposema kuwa “ugumu hutokana na shida ya kupata
neno mwafaka katika lugha lengwa kwa kuzingatia utamaduni wa dhana hiyo kwa
lugha chasili, matokeo ya kweli ni kuwa lugha mbili huwa na maana tofauti
kidesturi na kitamaduni.”
Kuna misingi
miwili ya kuhakiki kazi yoyote ya tafsiri. Msingi wa kwanza ni uelewa au ujuzi.
Tafsiri inatakiwa ionyeshe uelewa na ujuzi wa tamaduni tofauti. Msingi wa pili
ni `sababu` au lengo la mtunzi asilia ambalo linafaa kudhihirika katika matini
lengwa. Nahau, sawia na semi, hubuniwa kutokana na itikadi, mila, desturi na
mazingira ya watumizi wa lugha husika. Kipengele hiki cha utamaduni huwa muhimu
sana katika tafsiri. Hii ina maana kuwa nahau katika matini chasili
zinapotafsiriwa sharti mtafsiri azingatie utamaduni wa lugha lengwa. Yaani,
utamaduni wa lugha chasili na lugha pokezi huzingatiwa. Hii ni kutokana na
sababu kwamba lugha chasili na lugha pokezi zina tamaduni zao za kipekee na
ambazo zinatofautiana kwa kiwango kikubwa mno.
Imechangia
kuwepo kwa tanzu mpya na za kigeni katika fasihi ya Kiswahili. Awali Waafrika
waliidhamini sana fasihi simulizi. Hii ndiyo iliyokuwa fasihi yao. Hata hivyo,
tafsiri imesaidia kuingiza utanzu mpya katika fasihi andishi ya Kiswahili,
kwani historia ya fasihi barani Afrika inaonesha kwamba, hapo awali jamii za
kiafrika hazikuwa na utanzu huu wa fasihi. Hivyo basi, kupitia tafsiri fasihi
ya Kiswahili imeweza kujitanua zaidi.
Isitoshe,
tafsiri imesaidia kukuza na kusambaza fasihi ya Kiswahili ulimwenguni. Kwa
mfano Kiswahili kwenda lugha nyingine kama vile, Kijerumani “Kasri ya Mwinyi
Fuad” (Dei Sklaverei der Gewiirze) iliyotafsiriwa na Manique Lutgens na Karin
Boden (1997) miongoni mwa kazi nyingi zilizotajwa awali.
Historia ya
jamii husika hueleweka kupitia kazi za tafsiri. Katika tamthilia ya Nitaolewa Nikipenda kwa mfano, tunaona
historia ya taifa la Kenya tangu wakati wa ukoloni hadi wakati wa uhuru. Kwa
hiyo hapa tunaelewa yale yote wananchi wa Kenya walipitia wakati wa ukoloni,
kwa mfano katika uk. 32 mwandishi anaonesha adha walizopitia wananchi wa Kenya
katika harakati za kupigania uhuru na baadaye wakafanikiwa.
Vilevile
tafsiri husaidia kukuza fasihi ya lugha lengwa. Kupitia tafsiri fasihi ya lugha
lengwa inanufaika na kuingizwa vipengele kadhaa vya lugha hususani misemo au
methali ambazo hazikuwepo katika lugha lengwa. Kwa hivyo, kwa kutafsiri misemo
hii lugha lengwa nayo pia itakuwa imenufaika na misemo hiyo, kwa mfano, katika
“Nitaolewa Nikipenda”, msemo; “when axes are kept in a one basket they must
necessarily knock agaist each other” umetafsiriwa kama;“vyuma vikiwa katika gunia moja havikosi kugongana” uk. 24.
Kwa hiyo tunaweza kuwa tumeongeza msemo mwingine katika Kiswahili kupitia
tafsiri hii.
Pia tafsiri
hutusaidia kujua itikadi ya mwandishi na pengine itikadi ya jamii husika. Kwa
muktadha wa tamthilia hii tunaona mwandishi, anapinga sana tamaduni na mtindo
wa maisha ya kimagharibi ikiwa ni pamoja na dini za kigeni, lugha zao na mambo
yote yaliyoletwa na wakoloni, uk. 5.
Ukitazama
kwenye uga wa fasihi simulizi, utagundua kwamba tanzu zote za fasihi simulizi
zimetafsiriwa katika lugha mbalimbali
ili kukidhi haja ya jamii lengwa. Tafsiri hizi sio tu kutoka aidha Kiingereza
hadi Kiswahili la hasha! Zipo kazi chungu nzima ambazo zimetafsiriwa zikiwa ni
pamoja na hadithi za aina mbalimbali ambazo zimetafsiriwa kutoka lugha ya
Kiswahili hadi lugha za kiasili.
Mfano
mwafaka ni hadithi ambazo ni khurafa,
hekaya, mighani, mazimwi, ambazo kwazo tunaweza kuzipata katika lugha tofauti
tofauti kulingana na malengo ya mtafsiri na mtafsiriwa. Mfano tu mwafaka ni
aina mbalimbali za kharafa ambazo zimetawala kwenye maandishi mengi sana ya
fasihi simulizi ikiwa ni pamoja na Kichicheo cha Fasihi simulizi cha Wamitila ,
Fasihi simulizi kwa shule za sekondari pamoja na Msingi wa Fasihi simulizi cha
Kitula Kinge’ei na Catherine N.M. Kisovi. Machapishi haya yamebeba kazi
chungunzima ambayo baadhi imetafsiriwa kutoka lugha mbalimbali hadi Kiswahili
au lugha za asili.
Changamoto
katika kutafsiri matini za kifasihi ima andishi au simulizi
Tafsiri hizi
hata hivyo zimeandamwa na changamoto si haba katika kuhakikisha kuwa tunapata tafsiri faafu
za kazi za lugha ya kigeni.
a.
Kwanza kabisa ni muhimu kufahamu kuwa, matini
za kifasihi huwa tofauti kabisa na matini nyingine. Lugha ya kifasihi huwa
tofauti kabisa na lugha ya kawaida na hii ndio haswa husababisha kuwapo na
changamoto. Lugha ya kifasihi imetawaliwa na misemo, nahau, methali na
tamathali za semi, vipengele hivi kimsingi ndio huunda lugha ya kifasihi. Na
kwa hiyo mfasiri anapokuwa katika mchakato wa kufasiri matini za kifashi ni
lazima akumbane na changamoto katika kufasiri vipengele hivi. Kwa mfano anaweza
kukutana na methali au msemo ambao haupo katika lugha lengwa kwa hiyo katika
mchakato wa kufasiri anaweza kukosa kisawe cha methali au msemo huo katika
lugha lengwa na akaishia kufasiri kisisisi au kutumia kisawe ambacho hupotosha
maana. Kwa mfano, methali “A rich man’s fart does not stink” imetafsriwa kama
“Mashuzi ya tajiri hayachukizi”. Mfasiri alipata ugumu katika kufasiri methali
hii ndio maana akaamua kufasiri kisisisi. Ikiwa mfasiri hatokuwa na taaluma ya
kutosha juu ya fasihi, hataweza kufasiri kwa ufasaha misemo, mafumbo, nahau,
tamathali za semi na hata miundo na mitindo inayotumika katika kazi husika, kwa
hiyo kufasiri matini za kifasihi pia huhitaji utaalamu katika uwanja huo.
b.
Changamoto nyingine ni tofauti za
kiutamaduni. Mambo kama dini, mavazi, mila na desturi. Kwa mfano, majina ya
Kirusi huwa na maana yenye ujumbe mahususi, hivyo yanapofasiriwa katika
Kiswahili hupoteza ile maana halisi na kupotosha ujumbe uliokusudiwa.
c.
Vilevile changamoto ya tofauti za kiisimu
baina ya lugha mbili katika muundo wa sentensi na maumbo ya maneno. Kwa mfano
muundo wa Kiingereza ni tofauti na muundo wa Kiswahili. Kuna maneno mengine
ambayo sio rahisi kupata kisawe chake katika lugha nyingine, kwa hiyo mfasiri
anapokutana na maneno kama hayo hupata changamoto kubwa.
d.
Pia changamoto nyingine ni kutoelewa mbinu
mwafaka ya tafsiri husika, hivyo husababisha tafsiri kuwa tenge/mbovu. Hivyo
basi, ni dhahiri kwamba si rahisi kupata tafsiri iliyosahihi kwa asilimia zote,
isipokuwa tunaweza kupata tafsiri bora kama tu wafasiri wa kazi za kifasihi
watakuwa na sifa stahiki. Kwa mfano, uwezo wa kumudu lugha, kujua utamaduni wa
lugha husika pamoja na mazingira yake, kuwa na ujuzi wa taaluma husika kabla ya
kufasiri nk.
e.
Kwa upande mwingine, ushairi ni utanzu
unaokabiliwa na changamoto nyingi zaidi katika kufasiri kutokana na kwamba, kwa
kiasi kikubwa ushairi hutumia lugha ya mkato na ya kisanaa zaidi yenye msamiati
mgumu uliosheheni taswira, ishara, lahaja, tamathali za semi pamoja na misemo,
mafumbo nk. Hivyo basi, kuna uwezekano mkubwa wa kupotosha maana ya kifasihi
pamoja na sanaa iliyomo katika utanzu huu. Licha ya hayo, vilevile ugumu
unasababishwa na kanuni za kiarudhi hasa katika mashairi ya kimapokeo kwani, ni
vigumu sana kutafsiri ushairi huku ukizingatia urari wa vina na mizani bila kupotosha
maana iliyokusudiwa.Upotoshaji wa kipengele cha mtindo ni tatizo lingine.
Matini mengi ya kiingereza hasa hutumia neno “ACT” Neno hili hufasiriwa kama
onyesho na vilevile kama tendo. Upotoshaji huu huleta mkanganyo hasa kwa
msomaji wa matini pokezi. Huifanya hadhira ifikiri kwamba hivi ni vitabu viwili
tofauti. Jalada ni sula jingine. Upotoshaji wa jalada la kitabu hufanyika
kutokana na utamaduni wa lugha chanzi na lugha lengwa. Michoro hufanywa kwa
kuzingatia kipengele cha utamaduni.
Suluhisho la changamoto
hizi.
Changamoto hizi zote zinaweza
kukabiliwa tu ikiwa;
·
Mtafsiri atakuwa na umahiri wa lugha zote.
·
Atazielewa tamaduni za jamii hizi.
·
Atafahamu mazingira ya tamaduni zote mbili.
·
Atajua lengo au dhamira ya mwandishi wa
matini chanzi.
Hitimisho.
Kimuhtasari,
makala hii imedadisi mchango wa kazi zilizotafsiriwa katika kuendeleza lugha na
fasihi hasa simulizi ya Kiswahili pamoja
na kuchanganua changamoto zinazoambatana na tafsiri hizi. Imedhihirika wazi
kuwa ipo haja ya kuzidhamini kazi hizi, kuzichunguza upya tena kwa nia ya
kuzikosoa na zaidi ya yote kupendekeza njia mwafaka za kuibuka na tafsiri faafu
katika karne hii ya teknolojia na utandawazi.
MAREJELEO
a.
Catford, J. (1965). Linguistic Theory of
Translation. London: Oxford University Press.
b.
Crystal, D. (1987). Encyclopedia of Language.
Cambridge: Cambridge University Press.
c.
Larson, M. (1994). “Translation and
Linguistic Theory” An article in the Encyclopedia of Language and Linguistics.
Vol.9 Pergamon Press Oxford.
d.
Mwansoko, H. (1996). Kitangulizi cha Tafsiri: Nadharia na Mbinu.
Dar-es- Salaam: TUKI.
e. Munday, J.
(2001). Introducing Translation
Studies: Theories and Application. London: Routledge.
f.
Newmark, P. (1981): Aproaches to Translation.
Oxford: London.
g.
Nida, E. (1964). Toward a Science of
Translating. Leiden: E. J. Brill.
h.
Omboga, Z. (1986). Fasihi Tafsiri katika
Ukuzaji wa Fasihi ya Kiswahili: Matatizo na Athari zake. Unpublished M.A
Dissertation, Nairobi University.
i.
Teilanyo, D. (2007). `Culture in Translation:
The Example of J.P. Clark`s The Ozidi Saga` in Babel, Vol:53, Issue:1. Pg.
79-82.
j.
TUKI, (2004).
Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Nairobi: Oxford University Press.
k.
TUKI, (2006). English-Swahili Dictionary.
Dar-es-Salaam: TUKI
l.
Wanjala S. F (2011) Misingi ya ukalimani na
tafsiri; Serengeti Education publisher (T) L.T.D. Mwanza Tanzania
m. Method,
S.(2015).Umahiri Katika Fasihi ya Kiswahi, Mwongozo Kwa Mwanafunzi na
Mwalimu wa Fasihi Simulizi na Andishi. Meveli Publishers (MVP).
n. Ruhumbika,
G. (1978). Tafsiri za kigeni katika ukuzaji wa fasihi ya Kiswahili.
Makala.
o. Wafula,
R.M (1999).Uhakiki wa tamtiliya, Historian a maendleo yake . Nairobi
Kenya: Jomo Kenyatta Foundation.