Monday

neno ndicho kipashio cha msingi cha semantiki

0 comments

 

JADILI KAULI KUWA NENO NDICHO KIPASHIO CHA KIMSINGI CHA SEMANTIKI

TUKI (2004) wanadai kuwa neno kama kipashio cha usemaji ambacho hujengwa na mwanadamu au mkururo wa sauti zilizopangika kisilabi na ambazo hutambuliwa na wasemaji wa lugha inahusika kuwa kitu kimoja chenye maana mahususi.

Naye Mdee (2010:5) anafasili neno kwamba ni mfululizo wa herufi ulioafungamana pamoja na kuzungukwa na nafasi tupu. Pia Kihore na wenzake (2001) wanafasili neno kwa kutulia maanani maelezo ya Lyons (1984:194-208) kuwa neno linaweza kufafanuliwa katika misingi ya kiumbo-sauti (yaani, kwa kuchunguza sauti zinazounda umbo zima), kiotografia (yaani kwa kuchunguza herufi zinazotumika katika kuliundika umbo lake) na kisarufi (yaani, kwa kuchunguza kilekinachowakilishwa na umbo husika katika lugha).

Spencer(1991:41) anafafanua kuwa dhana ya neno ni dhana tata sana japokuwa   ni dhana muhimu sana katika nadharia za mofolojia.Wataalamu mbalimbali wamejaribu kufasili neno lakini kila nadharia waliyoitumia kufasili neno  haikukidhi kueleza  neno ni nini hasa ukitofautisha na dhana nyingine kama leksikoni. Njia mojawapo ya kufasili neno ni kwa kuangalia sifa zake kiisimu yaani kifonolojia, kimofolojia na kisemantiki. Ikiwa kigezo hiki kitatumika  kwa lugha moja moja huweza kuwa na mafanikio lakini tatizo kubwa ni kupata vigezo majumui vitakavyokidhi lugha zote.

Katamba (1993:17) anadai kuwa wazo kuwa lugha huundwa na maneno huchukuliwa kwa mazoea ya watu wengi kwani hata mtu asiyejua kusoma na kuandika anatambua kuwa kuna maneno katika lugha yake. Kumekuwa na mawazo tofautitofauti juu ya neno hasa ni nini. Dhana ya neno hutumiwa katika fahiwa mbalimbali ambazo ni vigumu kuzitofautisha.

Mdee (2006:5) anadai kuwa umbo linalojulikana katika lugha ya kawaida kama neno lina utata kwani ni umbo lenye sura nyingi. Utata huu unatokana na mitazamo tofauti ya wanaisimu kuhusu kipashio hiki kitahajia, kimatamshi,na kimaana.

Kamusi ya Kiswahili Sanifu (toleo la tatu, 2013:420) wametoa fasili tatu za neno. Fasili ya kwanza “neno” limefasiliwa kama mkusanyiko wa sauti zinazotamkwa au kuandikwa pamoja na kuleta maana. Kisha wakafasili neno kama jambo kubwa  mfano nina “neno” nataka kukupa; ameniletea neno, na katika fasili ya tatu wamefasili neno kama mahubiri, mfano “neno” la Mungu.

Kwa mujibu wa Longman Dictionary (2008:1899) wamefasili neno  kama kipashio cha lugha ambacho mtu anaweza akaelewa iwapo kitakuwa kimesemwa au kuandikwa kama kilivyo. (tafsiri yetu)

Habwe na Karanja (2004:71) wanasema neno ni kipashio cha kiisimu kinachoundwa na mofimu moja au zaidi.

Katamba (1994:38) anasema neno ni kipashio kidogo cha maana katika lugha ambacho kina dhima ya kisarufi. Anaendelea kusema, neno linaweza kusimama peke na kuleta maana bila kupachikwa vipande vingine. Hivyo katika neno “childish” (utoto) linaweza kutenganishwa na kubaki “child” (mtoto) na neno hili likatumika kiupwekeupweke kwa sababu ni neno linalojitegemea. Lakini hatuwezi kutenganisha kipande “ish” kikasimama pekeyake na kuleta maana.

Kutokana na maelezo haya basi  neno ni kipashio cha lugha kinachoundwa na mofu moja au zaidi ambayo inaweza kusimama peke yake na kuleta maana katika lugha mahususi.

Ni kweli dhana ya neno ina utata. Utata huo unasabishwa na vigezo tofautitofauti ambavyo hutumika katika kufasili dhana ya neno na mipaka yake.

Mdee (2010:5) anafafanua njia tatu zinaweza kutumika katika kufasili neno, njia hizo ni kama:- neno kama kipashio huru kisichogawanyika; maana ya neno kiothografia, na neno kama kipashio cha maana. Sisi tumeenda mbali kwa kuongeza fasili nyingine za neno kwa vigezo kama vile kigezo cha kisarufi katika kufasili dhana ya neno na kigezo cha kifonolojia.

Neno kama kipashio huru kisichogawanyika.

Fasili hii ya neno ni ya Leonard Bloomfield (1933) inayosema “neno ni umbo dogo kabisa lililo huru”. Fasili hii ina mambo makuu mawili, kwanza neno liwe umbo dogo, pili neno liwe umbo huru. Hapa umbo dogo humaanisha umbo ambalo haliwezi kugawanyika bila kupoteza maana yake. Mfano neno “pasi” huwezi kuligawanya katika “pa” na “si” bila kupoteza maana yake. Hivyo umbo dogo ni lile ambalo linashikilia maana. Kwa upande wa neno kuwa huru ina maanisha umbo hilo lazima liweze kutamkwa pekee bila kutegemea au kuliambisha kwenye neno lingine, haya ni maneno kama vile njooletejua, n.k.

Tatizo(utata) la kigezo hiki:

Ugumu wa kigezo hiki neno linalopewa uzito hapa ni lile katika lugha za mazungumzo pekee. Katika lugha za maandishi tunaweza kuwa na vipande vidogo vya maneno lakini ambavyo vikiwa huru hatuwezi kusema vina maana kwa kuwa huwa havirejelei kitu au hali yoyote ile. Mfano katika lugha ya Kiswahili vipande “na”, “kwa”, “tu”, n.k havina maana vikiwa pekee pekee. Katika lugha ya Kiingeza vipande kama “a”, “the”, “and”, “to”, n.k vivyo hivyo havina maana vikiwa pekee pekee.

Maana ya neno kiothografia.

Kigezo hiki huchukulia neno kuwa ni maandishi yanayoacha nafasi mwishoni. Rubanza(2010), anaeleza kwamba neno kiothografia ni mfuatano wa maandishi ambao huacha nafasi tupu mwishoni bila uwepo wa nafasi tupu katikati. Neno hudhiirika linapokuwa katika maandishi tu na lisiwe na nafasi katikati. Mfano; ubaochaki n.k. Maneno kama Askari kanzuBata maji, n.k huchukuliwa kama maneno mawili tofauti. Katika Kiingereza neno kama “cannot”, “blackboard”, n.k huchukuliwa kama neno moja. Maneno kama “washing machine” (mashine ya kufulia) na “White House” (ikilu ya marekani) huchukuliwa kama maneno mawili tofauti.

Matatatizo ya kigezo hiki: 

Hushidwa kuelezea maneno ambatani, kwao uandikaji wa neno ambatani kwa kutenga au kuacha nafasi katikati huchukulia kuwa ni maneno mawili. Hii sio sahihi kwani maneno ambatani huwa na dhana moja hivyo hutakiwa kuchukuliwa kama neno moja. Pia kigezo hiki hushughuliki tu na lugha ya maandishi na kuipuuza lugha ya mazungumzo ambayo ndiyo hutupatia lugha ya maandishi. Pia zipo kugha nyingine ambazo hazitengi maneno yake katika uandishi, pamoja ya kuwa ndani ya neno moja kunaweza kuwa na dhana nyingi zinazorejelewa. Mfano lugha ya Kigreenland Eskimo neno “uluminippug” maana yake ni “yumo mwanaume ndani ya nyumba yake”.


Dhana ya neno kifonolojia.

Kigezo hiki huchukulia neno kuwa ni kipande cha lugha kinachotokana au kujengwa na kipashio kidogo cha kimatamshi. Kufuatana na kigezo hiki kuna vigezo fulani vilivyo wekwa ambavyo hutofautiana kutoka lugha moja na nyingine. Rubanza (ameshatajwa) hueleza kwamba zipo lugha ambazo upo uwezekano wa kulitambua neno kwa kutumia sifa za kimatamshi. Lugha kama hizi ni zile ambazo zina utaratibu wa kuweka mkazo mahali fulani maalumu katika maneno wakati wote. Anaeleza zaidi kwamba sehemu hiyo inaweza kuwa mwanzoni mwa kila silabi ya kwanza ya neno, au silabi ya pili toka mwisho kwa baadhi ya lugha. Kwa mfano chunguza sentensi ifuatayo kutoka katika lugha ya Kingereza; “I didn’t take the test yesterday” Kufutana na utaratibu wa lugha hii sentesi hii ina maneno matatu tu yaliyokolezwa, kwasababu mkazo huwekwa kwenye maneno yenye kubeba maana (content words). Utaratibu huu una vighairi kwa sababu kuna wakati hata yale maneno yasiyobeba maana (grammatical words) hubeba mkazo kwa sababu za kimsisitizo wa neno au maneno husika katika sentensi (prosodic stress) Mfano katika sentensi ilele “I didn’t take the test yesterday” Ikiwa mzungumzaji ataweka mkazo kwenye “I” atakuwa akionyesha msisitizo sio yeye aliyefanya jaribio jana. Ikiwa mzungumzaji ataweka mkazo kwenye “didn’t”atakuwa anasisitiza kuwa yeye hakufanya jaribio jana (labda kafanya jambo jingine). Na ikiwa mzungumzaji ataamua kuweka mkazo kwenye “the” atakuwa akimaanisha kuwa hakufanya jaribio hilo(linalokusudiwa na muulizaji) labda kafanya jaribio lingine tofauti.


Hivyo kwa kutumia kigezo cha mkazo katika maneno tunashindwa kufahamu neno hasa ni lipi. Je vile vipande vya sauti ambayo havibebi maana katika lugha basi navyo ni maneno? Na kama ndio, basi kwa nini lugha hii isivitambue kama ni maneno kamili kiasi cha kubeba mkazo asilia?


Dhana ya neno kwa kigezo cha maana.

Kwa mujibu wa Mdee (ameshatajwa) hueleza kwamba neno ni kipashio kidogo cha lugha chenye maana, hueleza zaidi kwamba neno ni lazima liwe na maana. Mfano; baba – mzazi wa kiume, mama – mzazi wa kike. Kwa hiyo kwa kutumia kigezo hiki neno hutambuliwa kuwa ni kipashio cha kiisimu chenye maana.

Utata wa kigezo hiki: Je, maneno yote ya lugha yana maana ya kisemantiki? Pia kuna maneno mawili au zaidi yenye maana moja, Kwa mfano; mkono wa birika, maana yake mchoyo. Yapo maneno mengine yenye maana zaidi ya moja, mfano; kaapaa, na kata, maneno haya yakisimama yenyewe huwezi kupata maana moja mpaka yawe katika mahusiano na maneno mengine kwenye sentensi.

Dhana ya neno kisarufi.

Kwa mujibu wa Katamba (1993:19) ili neno litambulike lazima liwe katika muktadha wa matumizi. Katamba, anasema neno moja linaweza kuwa na dhima mbalimbali na dhima hiyo itagundulika tu litakapokuwa ndani ya muktadha wa matumizi kwenye sentensi. Anatoa mtano wa neno la kiiingereza “cut” kwamba likiwa kiupweke upweke mtu hawezi kutambua linarejelea nini, pamoja kwamba neno hilo katika lugha ya Kiingereza ni kitenzi yaani “kata” lakini kuna wakati linaweza kutumika kurejelea nomino. Chunguza mifano hii: “I need my cut” na “I have cut my finger”. Ukiichunguza vizuri mifano hii “cut” katika sentensi ya kwanza hurejelea nomino yaani “nahitaji stahiki yangu”(tafsiri yetu)  na “cut” katika sentensi inayofuata hurejelea kitenzi yaani “nimekata kidole changu”.

 Kigezo hiki pia huenda mbali kwa kufafanua kuwa pia maneno kama; natu,si, n.k katika Kiswahili na maneno; andanthe, on n.k katika Kiingereza nayo hayawezi kutambulika yanarejelea nini lazima yawe katika muktadha wa matumizi ndio tunaweza kusema ni aina gani za maneno au kutambua maana zake.

Udhaifu wa kigezo hiki ni kwamba kuna maneno mengi sana ambayo maana zake hutambulika hata yasipokuwa katika muktadha wa matumizi kwenye sentensi, aya au kifungu cha habari. Maneno haya ni kama vile nomino za mahali kama vile Dar es Salaam, UlayaBukoba n.k; nomono za pekee zinazorejelea majina ya watu kama vileMutashobyaMwendamsekeRubanza, n.k. Sasa tunajiuliza kuwa aina hizi za nomino na nyingine nyingi ambazo ni kama hizi je si maneno? Hivyo na kigezo hiki hakijajitosheleza katika kutupatia maana ya “neno” itakayokidhi mahitaji ya taaluma zote.

Kwa hivyo kutoka na makala haya ni kuwa kwa vile semantiki ni tawi la isimu ambalo linashughulikia matumizi ya lugha katika awamu mbalimbali na neno likiwa mojawapo wa viambajengo hivi, neno linakuwa nguzo na msingi katika tawi hili. Neno linakuwa na nafasi ya kimsingi ni wazi kwamba suala hili zima linajengeka kwenye misingi ya neno.

Kimsingi neno linaweza kujitokeza  kama  mofu, au mofimu linapotekezea majukumu yake.

 

 

Neno kama mofu.

TUKI(1990), katika Dafina ya Lugha wanasema kuwa, “Mofu ni kipashio cha isimu maumbo kiwakilishacho mofimu”. Massamba (2004), katika Dafina ya Lugha anasema , Mofu ni kipashio cha kimaumbo ambacho huwakilisha mofimu. Kwa mujibu wa Nida (1949), wanasema, Mofu ni umbo la neno ambalo huwakilisha mofimu na ambalo huthihirika kifonolojia na kiothografia. Mofu ni kipashio kidogo kabisa chenye maana katika lugha.Mofu hawezi kugawanywa katika sehemu ndogo zaidi bila kuharibu maana yake. Mofu huwakilisha maana za kileksika na zile za kisarufi. (Platt,1985). Kwa ujumla, Mofu ni kipashio cha kimofolojia ambacho husitiri maana za mofimu katika lugha na huweza kudhihilika kifonolojia zinapotamkwa na kiothografia zinapoandikwa katika lugha. Mofu huainishwa kwa kuzingatia vigezo viwili; Kigezo cha maana zinazowakilishwa na mofu na Kigezo cha mofolojia ya mofu.

Mofu huainishwa kwa kuzingatia vigezo viwili:

(i)     Kigezo cha maana zinazowakilishwa na mofu;

(ii)    Kigezo cha mofolojia ya mofu.

Tunapotumia kigezo cha maana zinazowakilishwa na mofu, tunapata aina tatu za mofu, yaani:

 (i)    Mofu huru

 (ii)   Mofu funge

 (iii) Mofu tata

Kwa upande mwingine tunapotumia kigezo cha mofolojia au maumbo ya mofu zenyewe tunapata aina mbili za mofu, yaani:

(i)     Mofu changamano

(ii)    Mofu kapa

 

Kwa mantiki hii tunazo aina tano za mofu ambazo ni:

(i)     Mofu huru

(ii)    Mofu funge

(iii)  Mofu tata

(iv)   Mofu-changamano

 

(i)     Mofu Huru

Mofu huru ni zile mofu ambazo zinaweza kukaa peke yake kama maneno kamili yenye maana inayoweza kueleweka bila kusaidiwa na mofu nyingine. Aghalabu, mifano mingi ya mofu huru hupatikana kutoka kwenye vipashio vya lugha, kama ifuatavyo:

 

(a)       Nomino:  {baba}, {kuku}, {sungura}, {ndege}, {dada}, {paka}, nk.

 

(b)       Vivumishi: {safi}, {baya}, {dhaifu}, {zuri}, {imara}, {hodari}, nk.

 

(c)       Viwakilishi:{mimi}, {sisi}, {wewe}, {ninyi}, {yeye), {wao}, nk.

 

(d)       Vielezi:  {upesi}, {haraka}, {sana}, {leo},          {jana}, {juzi}, nk.

 

(e)       Vitenzi: {tafiti}, {samehe}, {arifu}, {sali},         {jibu}, {badili}, nk.

 

(f)        Vihusishi: {ya}, {juu}, {mbele}, {kwa}, nk.

(g)       Viunganishi:{na},{halafu}, {bado}, {ila}, {aidha},{pia}, nk.

Kwa mujibu wa mifano hii inadhihirika kwamba Kiswahili kinazo mofu huru nyingi ambazo zimo katika aina zote za vipashio vya lugha. Hivyo, mofu huru ni mofu ambazo zinaweza kukaa peke yake kama maneno kamili yanayoeleweka bila kusaidiwa na viambishi.

 

(ii)       Mofu funge au Mofu tegemezi

Mofu funge au Mofu tegemezi ni mofu ambayo haiwezi kutumiwa peke yake kama neno lililo na maana yake kamili; aghalabu mofu funge hutumiwa kama kiambishi tu kinachoambatanishwa na mzizi au viambishi vingine ili kulikamilisha neno husika. Mofu funge ina sifa zake ambazo ni pamoja na:

 

(a)    Mofu funge haiwezi kukaa peke yake ikawa neno kamili.

 

(b)    Mofu funge ni lazima iambatanishwe na angalau mafu nyingine moja ndipo tupate neno kamili.

 

         Kutokana na sifa hii ndiyo mdiyo maana wanaisimu wengine huziita mofu hizi kuwa ni mofu tegemezi ambayo ina maana sawa na mofu funge


Neno kama mofimu

Mofimu ni vipashio vinavyoonyesha uhusiano uliopo kati ya sauti-msingi za lugha (yaani fonimu) na maana maalumu katika sarufi ya lugha. Hivyo tunaweza kusema kuwa mofimu ya umoja katika neno {mtu} imeundwa na fonimu /m/ ambayo ni king’ong’o cha mdomo; na mofimu ya wingi imeundwa na fonimu mbili /w,a/ ambazo ni kiyeyusho na irabu chini. Sasa bila shaka unaweza kuona uhusiano uliopo kati ya vipashio vya kifonolojia tulivyojadili katika sura ilyotangulia, na uundaji wa mofimu za lugha.

Kila neno katika lugha limejengwa na mofimu moja au zaidi. Neno linalojengwa na mofimu moja tu linaitwa neno sahili, na lile linalojengwa na mofimu zaidi ya moja linaitwa neno changamano. Hivyo, katika Kiswahili, tunaweza kusema kuwa {chungwa} ni neno sahili kwa vile haliwezi kukatwakatwa katika vipashio vidogo zaidi, kama tukilinganisha {chungwa: machungwa}.

Maneno yaliyo mengi katika lugha kama ya Kiswahili ni changamano kama itakavyodhihirika katika mifano. Hata maneno mafupi kama {wa, ya, vya} ya sentensi za (4) hapo juu, ni changamano. Kila moja lina mofimu mbili, moja ambayo inasimamia upatanisho na nomino, na /-a/ ambayo haibadiliki, na katika sarufi ya Kiswahili tunaiita {-a} mofimu ya ‘uhusiano’. Lugha nyingine zinayo maneno sahili mengi zaidi ya Kiswahili. Katika lugha ya Kiingereza, kwa mfano, nomino nyingi katika umoja ni manerio sahili: {boy, girl, book} etc. Lakini, katika wingi, nomino nyingi za Kiingereza ni maneno changamano {boy-s, girl-s, book-s} etc. Hata vitenzi vya Kiswahili si maneno sahili hata kama hayajaambikwa vipashio vingine. Kwa mfano neno {sema}:

8 a) Juma amesema wageni wamekuja


b) Juma hasemi uwongo.

Kipashio /sem-/ katika sentensi hizo ni mzizi wa kitenzi {sema}, kwa sababu ndiyo sehemu ambayo haibadiliki, na hivyo tunaona kuwa fonimu /a/ ya {sema} si sebemu ya mzizi wa kitenzi hicho kwa sababu inaweza kudondoshwa na nafasi yake ikacbukuliwa na kinashio kingine kama hapo juu. Hata hivyo tunaweza kupata maneno zaidi ya Kiswahili ambayo ni sahili, kama vile maneno ya sifa: {safi, kubwa, dogo, fupi; zuri} n.k. (mfamo:{chungwa safi, kubwa, zuri} n.k.

Neno changamano linaundwa na aina mbili za mofimu: 

mzizi na kiambishi (au viambishi); ambapo neno sahili linaundwa na mzizi peke yake. Viambishi viko vya aina tatu: viambishi-tangulizi, vinavyoambikwa kabla ya mzizi wa neno; viambishi-fuatishi, vinavyoambikwa baada ya mzizi; na viambishi-kati, ambavyo vinaingizwa katika mzizi, na hivyo kuukata katika sehemu. /m/ na /wa/ katika maneno {m-tu} na {wa-tu} ni viambishi-tangulizi, ambapo /-i-/ na /-ish-/ katika maneno {kat-i-a} na {kat-ish-a) ni viambishi-fuatishi. Viambishi kati havitokei katika Kiswahili, lakini vipo katika lugha nyingine.

MAREJELEO.

Bloomfield, L. (1933). Language. Henry Holt: New York.

Habwe, J. na Karanja, P. (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Phonex Publisgers: Nairobi

Katamba, F. (1993). Morphology. Mac Millan Press Ltd: London

Katamba, F. (1994). English Words. Routledge: London

Mdee, S. (2010). Nadharia na Historia ya Leksikografia. TUKI: Dar es Salaam

Quirk, L. (2005). Longman Dictionary of Contemporary English. Pearson Longman: New York

Rubanza. (2010). basic Reading. Yaliyoandailwa na Rubanza.

TUKI (2013). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. (Toleo la tatu). Oxford: Dar es Salaam

Besha, R.M. (2007). Utangulizi wa Lugha na Isimu. Dar es Salaam: Macmillan Aidan Ltd.

Habwe, J. & Karanja, P. (2007). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers.

Katamba, F. (1993). Morphology. London: Macmillan Press Ltd.

Massamba, D.P.B  na Wenzake. (2013).  Fonolojia ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam: TUKI.

Matinde, R.S. (2012). Dafina ya Lugha Isimu na Nadharia: Kwa Sekondari, Vyuo vya Kati na   Vyuo Vikuu. Mwanza: Serengeti Educational Publishers (T) Ltd.

Mdee, D. (2007). Nadharia za Leksikografia. Dar es Salaam: TUKI.

TUKI. (1990). Kamusi ya Isimu na Lugha. Dar es Salaam: TUKI             

 

 

 

No comments:

Post a Comment