Monday

nadharia ya kiutanzu uhakiki wa tamthiliya ya pango

0 comments

 

Swali:  TUMIA NADHARIA YA KIUTANZU KUHAKIKI TAMTHILIA YA PANGO.

Hii ni nadharia ambayo inahusu ugawaji wa tanzu mbalimbali za fasihi katika makundi yake mahsusi. Katika nadharia hii huwa tunazama katika namna ya kujuana kufahamu utanzu ni nini? una sifa gani? unaweza kutumika kivipi ili kueleza usemaji mbalimbali.

Miongoni mwa waasisi wa nadharia hii ni Mgiriki Aristotle. Mgiriki huyu anatoa maoni kuwa utanzu huwa na sifa mahsusi hasa alipotazama na kusikiliza aina mbalimbali za fasihi. Katika utafiti wake huu, aligungua kuwa Wagiriki walikuwa na masimulizi maarufu ambayo waliyaita Tendi au Tenzi.

Waaidha walikuwa na nyimbo ambazo walipoziimba ziliambatana na firimbi, nzumari, zeze, kinubi, pembe n.k. Aliona vile vile Wagiriki walikuwa na maagizo ambayo yapo mengine yaliyohuzunisha mathalan msibahuku mengine yakichekesha yakimsawiri mwanadamu katika ubaradhuli na uduni wake. Kisha kulikuwa na yale yaliyokuwa ya mseto wa msiba na kuchekesha. Kwa Aristotle haya yalikuwa na sifa za kipeke zilizojitosheleza na mtunzi asingewezakutoka utanzu mmoja hadi mwingine.

Hata hivyo kuwa wataalamu kama Mikhail(Bakhtin) waligundua kwamba ni vigumu kwa utanzu kuwa  na upekee usioingiliana na utanzu mwingine. Tanzu zinaweza kuingiliana, kutaguzana na vile vile tanzu ni nyumbufu na zinasheheni utelezi mkubwa.

Kwa mujibu wa maoni haya, mwandishi mmoja anaweza kuandika tamtilia moja ikahusisha hadithi na ushairi lakini ikabaki tamthilia tu. Vile vile utanzu kama riwaya huweza kuwa na hurafa, nyimbo,visasili,vitendawili na tanzu nyingine nyingi.

Na wakati utanzu mkubwa unameza tanzu ndogo ndogo, hizi tanzu ndogo ndogo hutumika kimtindo kufanikisha utanzu mkubwa. Kwa mfano:-Methali katika riwaya inaelezza kazi kwa ujumla na vile vile wimbo hufanya kazi hiyo ama utunzi huo kama simulio na kuhamisha wimbo.

Kuna mtaalamu David Cryig ambaye yeye anashughulikia, kuzaliwa, kukua,kunawiri, kudididmia na kutokomea kwa tanzu za fasihi. Anasema kuwa utanzu huzaliwa kutokana na tabaka la kuzalisha mali katika jamii.

Kama utanzu wa riwaya kimagharibi ulizalishwa na ubepari- mhusika mdogo anatupwa baharini kwa sababu amekuwa tajiri.

Katika tamthilia ya Pango iliyoandikwa na K.W. Wamitila, swala la nadharia ya kiutanzu linadhihirika wazi kabisa. Mtuzi huyu ameangazia tanzu aina ainati katika kazi yake ya fasihi licha ya kuwa tamthilia.

Utanzu ambao unadhihirika wazi hapa ni ule wa nyimbo ambao huwa mojawapo wa vipera vya fasihi simulizi. Kwa hakika nyimbo huwa sehemu muhimu sana ya jamiina ambapo huwa na malengo na maudhui maalum. katika Tamthilia ya Pango, utanzu huu umetumika katika muktadha aina ainati.

a)    Kunao wimbo unaoongozwa na Kibwana (uk. 36-37). Wimbo huu unalilia hali ya wakombozi kukosa misimamo imara wa kupigania haki yao ya uongozi.Hili bila shaka ni kundi ambalo linamwunga mkono Katango kijana ambaye amejibwaga ulingoni kumenyana vikali na Ngwese. Kibwana anasema hivi:

        Kibwana: ……………………tulibeba gogog hili la hatima yetu

                        tulipagaze mabegani kwa kujitolea

                         tulipofika katikatiya mto

                        baadhi wakakimbia

                        wakakimbia

                                      wakakimbia

                                               wakakimbia…………

b)    Wimbo mwingine umejitokeza kwenye uk. 38 na ambao unaongozwa na Ngoi.Wimbo huu ni  wa kumsifu Ngwese kuwa ndiye afaaye kuliongoza Pango. Kupitiakwa wimbo huu, tunaweza kuona kuwa wimbo huu umejawa na majisifu na majigambo chungu nzima hasa unapomlinganisha Ngwese na vitu mbalimbali.

Ngoi:  (Akiimba) Wa Ngwese yuko hapa, wa Ngwese

           Wa Ngwese kimbunga, yu hapa, wa Ngwese

           Wa Ngwese shoka la kuikata miti mikinda, wa Ngwese

           Wa Ngwese mti uko tayari, wa Ngwese

            Wa ngwese shoka tia mpini, wa Ngwese

           Wa ngwewe kelele kinapinda

                                  majani yakitutetemeshe

           Wa ngwese…….. bingwa wa Pango. 

c)    Katika onyesho la tatu, Mama ambaye ni mkewe Seki, anajikuta katika kuuimba wimbo(uk 55) Maudhui ya wimbo huu ni kumsuta mumewe(Seki) kwa kutupilia mbali,majukumu yake katika nyumba.Twafahamu kuwa nyimbo huweza kudhihirisha hisia alizo nazo Mwimbaji. Kwa kupitia wimbo huu, tunapata taswira ya sononeko tupu la Mama kuhusu mienendo ya mume wake. Waaidha anaonyesha kujuta mikononi mwa Seki kama mume wake. Anaimba hivi:

…………………. “uchungu huu uliokithiri

moyo una uchungu

siku hizi mumeamegeuka umande

jua lipigapo anajiweka upande

kazi hafanyi

lawama hakomi

kisha chakula adai………….”

Hapa tunapata kuwa Seki haachi pesa za matumizi ingawa ajapo nyumbani ataka kula! Iwapo atakosa chakula, atapandwa na wakwao hali ambayo imemkera na kumsononesha Mama pakubwa.

Wimbo huu vile vile unadhihirisha wazi kuwa wanawake wamedharauliwa na jamii. Kwenye huo wimbo Mama aimba:

                           …………wake tumedhalilishwa na kuteseka

kuni kutafuta na watoto juu migongoni

chakula kutafuta na kuandaa jikoni

huku wenzetu njia wanazishika

huku sisi na wana tunasakimu…………(uk 55-56)

 

 

d)     Utanzu huu vile vile unajitokeza kwenye onyesho la nne uk.88. Huu ni wimbo wa ukomboziwa Pango hasa baada ya Ngwese kugunduliwa hila zake. Kupitia kwenye wimbo huu, tunaweza kufahamu kuwa waliomwunga mkono sasa wamebadili misimamo wa na sasa wamekubali kumwunga mkono Katango kuwa Kiongozi wa Pango.Wimbo huu wasema:

    

                     sauti:       Kimbunga cha uongo ngo ngo

                                    Kimbunga chaharibuPango ngo ngo

Kimbunga Kumbuka njia ya mwongo

kimbunga alisema yote Katango!

Kimbunga hata mlinzi hulindwa!

Wanapouimba  wimbo huu, tunawaona wote wakishikana mikono wakiwa na furaha kubwa huku Katango akiinuliwa juu.

Ulumbi.

Hiki ni kipera cha fasihi simulizi ambachokimezama katika mkumbo wa mazungumzo. Utanzu huu umejitokeza wazi katika kazi hii.Hii inadhihirika wazi kwenye ukurasa wa 9 wakati Katango anapotoa kauli yake ya kuwarai wakazi hawa kumchagua kuwa Kiongozi wao. Kauli hii iliteka bakunja umati uliokuwa pale kabla ya Ngwese kupewa fursa ya kumwaga shindo lake.

Kwa hakika sifa hii ya lumbi wa Katango imetambulika na wengi katika tamthilia hii akiwemo Babu ambaye kwenye ukurasa wa 69 anasema hivi kwa kumjibu Susa:-

Babu:       (Kwa mshangao mkubwa) Unasema nini sasa?

                  Iweje Katango     asiongee na ni mlumbi maarufu kijijini?

Iweje kuwa haongei na ni bingwa wa kuyasanifu maneno?          Iweje?

Hali hii ilitokea baada ya kugunduliwa kuwa Katango ametiwa kitata asiweze kuongea tena.

Ni dhahiri shahiri kuwa Katango ameibuka kidedea katika fani hii ya ulumbi kwa kuwa bingwa wa kuyasarifu maneno maneno anapozungumza. Katango angemithilishwa na walumbi mahiri kama Martin Luther King Jr.(1929-1968), Barack Obama, John F. Kennedy(1917-1963) au P.L.O Lumumba hapa nchini Kenya hasa katika makala yake yenye mvuto kwa Uteuzi wa msamiati wenye mvuto wa kipeke hasa makala ya, The Tragedy of Africa.

Katango anazidi kuonyesha umahiri wake katika ulumbi anaposadiki na wanakijiji kwa kugunduliwa hila za Ngwese na sasa wanakubali kumwunga mkono kwa kusema hivi:-

                   Katango: ………… sasa macho tumeyafungua

sasa upofu tumeupofua

sasa vinywa tumefungua

maovu nayo tumeyafukua.

Kwa upande mwingine utanzu wa misemo na methali  vile vile zi metumika pakubwa katika tamthilia hii ya Pango. Methali huwa kielelezo cha jamii. Kupitia methali mmoja anaweza kuifahamu historia na mapisi ya jamii husika. Ipo mifano chungu nzima ya utanzu huu katika kazi hii.

Kunguru ni mwoga lakini hana kipara(uk 34)

Msemo huu umetumiwa na Mama ikishauri Katango ukiwana maana kuwa ajiepushe na maswalaya siasa kwani hayana mwisho mwema. Asionyeshe ubabe kilamahali hivyo awe kama kunguru ambaye licha ya uwoga wake wote kunguru hana kasoro wala cha kujutia.

 

Hujui mkia hauongozi kichwa.( uk 35)

Seki kwa upande wake naye anautumia msemo huu kwa Katango. Hapa Seki ambaye ni baba yake Katango ana maana kuwa Katango hawezi kupata fursa ya kuliongoza Pango kwa vyovyote kwani Pango liko mikononi mwa Ngwese.

Kuteleza sio kuanguka (uk 46)

Methali hii imetumiwa na Ngwese alipokuwa akijaribu kuwarai wanakijiji kumpa fursa nyingine ya kumchagua  kuliongoza Pango hata ingawa hakutekeleza wajibu wake ipaswavyo.Anajitetea kuwa bado kuna uwezekano wa yeye kuia bidii na kujitahidi akipewa awamu nyingine.

Ngwese anazisha kwa kutumia msemo:kibuyu hakivunjwi kwa kukosa maziwa, akiwa na maana kuwa kukosa kutimiza wajibu kwake kusiwe chanjo cha kumwangamiza kisiasa.

Uchngu wa kujifungua hauwazuii wanawake kushika

mimba.(uk 58)

Msemo huu umetumiwa na Babu alikuwa akijaribu kumpa Katango moyo na matumani kuwa hata baada ya Ngwese kuibuka mshindi katika Uchaguzi wa kuwakilishwa Pango bado ana nafasi ya kutwaa uongozi wa Pango kwa hivyo asife moyo hata kidogo.

Ngoma ya wana haikeshi.(uk 84)

Methali hii imetumiwa na Jitu 1. Jitu 1 ana maana kuwa wakati wa vijana kuongozwa bado na kwa hivyo swala ambalo vijana wanalidhania lakuongoza Pango ni ndoto za alinacha tu. Anaendelea kwa kusema kuwa , Hujasikia mshairi maarufu aliyesema Haile ngoma ya wana sijaona ikeshayo?

Utanzu mwingine ambao unadhihirika hapa ni fasihi ya ngoma au ngomezi. Katika jamii za kiafrika, ngoma ilichukuliwa kuwa nafasikubwa sana katika mawasiliano na burudani.

Katika tamthilia hii, ngoma zimetumika katika muktadha mbalimbali. Katika sehemu ya pili onyesho la kwanza(uk.36) ngoma inasikika ikipigwa na vijana wanaompigia debe Katango.

Kwa vijana ngoma hii ni ishara ya mabadiliko katika ulimwengusasa ikizingatiwa kuwa katika jamii zetu za kiafrika masogora walikuwa wale wakongwe waliobugia munyu si haba.

Katika onyesho la tatu sehemu ya tatu(uk 75), wapo watu kadhaa ambao wanacheza ngoma karibu na pango.Huenda ikawa wanasherehekeanna kufurahikia hali yao inavyowaendea vizuri hata kama wengi wanasota kitango malele.Katika onyesho la nne(uk 82) vile vile kazi inaanza kwa ngoma tele.

Utanzu wa ushairi nao pia haukuwachwa nyuma. katika uk 38 wimbo wa Ngoi unachukua muundo wa shairi laaina ya kikwamba. Hapa kila mstari/mshororo umeanza kwa neno moja ambalo ni WA NGWESE

Ngoi:  (Akiimba) Wa Ngwese yuko hapa, wa Ngwese

           Wa Ngwese kimbunga, yu hapa, wa Ngwese

           Wa Ngwese shoka la kuikata miti mikinda, wa Ngwese

           Wa Ngwese mti uko tayari, wa Ngwese

            Wa ngwese shoka tia mpini, wa Ngwese

           Wa ngwewe kelele kinapinda

                                  majani yakitutetemeshe

           Wa ngwese…….. bingwa wa Pango. 

 

Katika uk 79 kupitia kwenye sauti baada tu ya mtuo sauti inadhihirisha utanzu wa ushairi kwa kuanza kwa neno moja kisha kuzingatia vina vya kati ifaavyo(za)kunena haya:

 

Sauti:                  kisha nitauza,nitauza nipate dola

kisha nitauza,nitauza nipate doola

kisha nitauza,nitauza nipate pa..uni

kisha nitauza,nitauza nipate yuro

kisha nitauza,nitauza nipate yeeni!!!

Katika shairi hili inabainika wazi kuwa mwandishi amezama zii katika Mashairi aina ya kikwamba ambayo yamedhihirika wazi katika tamthilia hii.

Waaidha Kibwana anaidondosha mistari ya muundo wa ushairi(uk 88) ambapo anasema:

           Kibwana(Akimzomea Ngwese)

                           Weye kimbunga upigaye

                          Weye tufani ufagiaye

                           Weye dhoruba utakasaye

                          Umejua ni nani wa kututangua?

Utanzu mwingine ambao umetumika hapa ni hadithi. Aghalabu hadithi huwa nafasi kubwa na kiburudisho chenye mafunzo na maadili  chungu nzima. Katika tamthilia hii, mwandishi ametumia utanzu hii kupitia wahusika mbalimbali .

Katango kwenye uk.42 anatongoa hadithi aina ya khurafa ambapo anasimulia kuhusu wanyama walioamua kukichimba kisima baada ya ukame kutawala eneo lao. Kupitia kwenye hadithi hii inadhihirika wazi kuwa ukubwa si neno bali maarifa. Hii ni kwa sababu licha ya ukubwa wa wanyama kama ndovu, simba, twiga mbogo hawakuweza kuchimbua maji hadi akatokea sungura ambaye hakudhaniwa kufaulu kwa udogo wake.

Hadithi hii ni taswira au kiangaza mbele kuwa licha ya Ngwese na ubabe wake, hataweza kulikomboa pango bali ni Katango(sungura) ambaye hadhaniwi kwa kuwa mtoto na mdogo wa Busara.

Ukweli huu unadhihirika mwishoni mwa tanthilia wakati ambapo wakazi hawa wanaghairi misimamo wao na Kuamua kumwunga mkono Katango kwa kugundua kuwa hawana mustakabali mwema mikononi mwa Ngwese.

Maigizo vile vile yameangaziwa na mwandishi wa tamthilia hii ya Pango. Katika uk 52 Ngwese alipokuwa akizozana na Sakina kuhusu kwenda kutekeleza wajibu wa kikazi baada ya kuchaguliwa,anamwigiza Sakina namna alivyokuwa akimshauri.

 

Ngwese:(Akiigiza) Kipindi cha kazi! Kipindi cha kazi! (Anatembea huku na huku) Ni kweli nilisema ni kipindi cha kazi, lakini sikusema ni nani atakayeifanya hiyokazi, unasikia? Kimsingi wao ndiyo wanaotaka kuichapa hiyo kazi………

Utanzu mwingine ambao umetumika hapa ni ule wa mawaidha. Katika jamii zetu mawaidha yalitolewa na wakongwe au mtu aliyekupiku kwaumri na maarifa ya kimaisha na aliyeaminika kuwa na Busara.

Katika tamthilia wapo wahusika mbalimbali ambao wanajitikeza wazi kuwausia wahusika wengine. Kwa mfano katika uk. 57, Babu anamshauri Katango kwa kumpamatumaini ya kuzidi kupigana na kuona kuwa ndoto yake ya kuongozwa pango inatimia.

Babu:   Sikiliza Katango wangu, mwewe anapomchukua kuku   wako, humrushii mayai;maana ukifanya hivyo hutobaki na chochote. Ni muhimu uwe na matumaini……….. sote tuwe nayo(mtuo) Uovu na ubaya haufichiki Katango; na una mwisho pia;tutamjua huyo Ngwese hivi karibuni. Watu husema kuwa uyoga hutoa mahali sawa lakini sio uyoga wote uliwao; watu hutambua upi wa kuliwa naupi usioliwa.

Majigambo ni utanzu ambao kwa hakika umejitokeza katika tamthilia hii.Katika usanii huu, kuna pande mbili na kila upande unajipigia debe kuwa ndio unaofaa Kuamua misimamo wa kisiasa katika sehemu hii ya Pango. Pande hizi zinaongozwa na Katanga(kijana) na Ngwese(mzee)

Katika uk 42-45 kwenye ile hadithi ya Katango kuhusu wanyama tunaona kuwa kila Mnyama ajaye kukichimba kisima kila mmoja alijigamba namna alivyo na uwezo mkubwa. Hata hivyo Katango anatumia mfano huu wa kisa kujigamba kuwa udogo wake usichukuliwe kuwa Udhaifu bali ano uwezo wa kuiongoza sehemu hii ya Pango swa na sungura aliyewapiku wale wanyama wenye nguvu waliomtangulia kisha kushindwa kukichimba kisima.

Anapopata fursa kwa upande wake, Ngwese kwenye uk.48 anasema:

                           Ngwese:    (Kwa kujishasha)

Ndimi kimbunga nipigaye,

Ndimi tufani nifagiaye,

Ndimi dhoruba nitakasaye,

nani wa kunitangua?

            kijana?

Kupitia kwa usemi huu inadhihirika wazi kuwa Ngwese ana wingi wa majigambo kwa kujiona kuwa ni mtu mwenye nafasi akilinganishwa na Katanga ambaye bado hali yake ya kiuchumi bado nyembamba.

Hitimisho

Imedhhirika wazi kuwa katika Tamthilia hii ya Pango, mwandishi ameangazia nadharia ya kiutanzu ifaavyo. Amevishughulikia vipera mabalimbali vya fasihi ambavyo kwamba vina niaya kuikamilisha kiufundi kazi yake.

Ufundi kama huu huzidisha hamu ya kutaka kukisoma kitabu hiki kwa kuwa mabadiliko ya tanzu mbalimbali huondoa kutamaushwa unapoisoma tamthilia hii.

Marejeleo.

Wamitila K.W. (2002), Uhakiki wa Fasihi Simulizi. Misingi na Vipengele Vyake. Nairobi Phoenix Publishers Ltd.

____________________(2004), Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi. Nairobi: Focus Publications Ltd.

_____________  (2016) Pango. Nairobi :Focus Publishers Ltd, ,.

Topan Farouk M. (1975), Uchambuzi wa Maandishi ya Kiswahili. Dar es Salaam: Oxford University Press.

TUKI (1981),  Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam: Oxford.

Njogu K. na R.M Wafula (2007), Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: K.L.B

Ogechi N. O et al (2008), Nadharia katika Taaluma ya Kiswahili na Lugha za Kiafrika. Eldoret: Moi University Press.

Njogu, K & Rocha, C. (1999). Ufundishaji wa Fisihi: Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Msokile, M. (1993). Misingi ya Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: East African Educational Publishers.

Abedi, A. (1954). Sheria za Kutungu Meshairi na Diwani ya Amri. Nairobi: East African Literature Bureau.

Hussein, E. (1983). Hatua Mbalimbali za Kubuni na Kutunga Tamthilia Kufuatana na Misingi ya KiAristotle, Fssibi. Dar es Salaam: TUKI.

Kezilahabi, E. (1983). Uchunguzi katika Ushairi. Fesihi. Dar es Salaam: TUKI.

Madumulla, J. s. (2009). Riwaya ya Kiswshili: Nadharia, Historic na Misingi ya Uchambuzi. Nairobi: Phoenix.

Wamitila, K.W. (2003).  Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia.  Nairobi: Focus Books

 

No comments:

Post a Comment